Watu 151 wafa katika mkanyagano Korea Kusini

Muktasari:

  • Watu 151wamefariki dunia katika mkanyagano uliotokea wakati wa sherehe za Halloween mjini Seoul, Korea Kusini.

Dar es Salaam. Watu 151wamefariki dunia katika mkanyagano uliotokea wakati wa sherehe za Halloween mjini Seoul, Korea Kusini.

Vifo hivyo vimetokea Jumamosi Oktoba 29, 2022 usiku wakati umati mkubwa wa vijana waliokuwa wakisherehekea sikukuu ya Halloween huko mjini Seoul kunaswa na kukandamizwa katika uchochoro mwembamba.

Maofisa wanasema watu wengine 150 wamejeruhiwa katika mkasa huo mbaya kuwahi kutokea nchini Korea Kusini kwa miaka mingi.

Mkanyagano huo umetokea karibu na Hoteli ya Hamilton katika wilaya ya Itaewon ambayo ni maarufu kwa burudani za usiku huku idadi kubwa ya watu wakiwa wamekusanyika katika uchochoro mwembamba karibu na hoteli hiyo.

Sherehe hizo za Halloween zilikuwa ndio za kwanza kufanyika mjini Seoul ndani ya kipindi cha miaka mitatu baada ya Serikali kuondoa vizuizi vya Uviko-19.

Kwa mujibu wa maofisa wa zima moto watu waliendelea kumiminika kwenye uchochoro mwembamba ambao tayari ulikuwa umefurika ukuta hadi ukuta, wakati wengine waliokuwa juu ya barabara yenye mteremko wakianguka na kuwaangusha wengine.

Ofisa wa idara ya Zimamoto, Choi Seong-beom amesema "Idadi kubwa ya majeruhi ilitokana na wengi kukanyagwa wakati wa sherehe za Halloween," amesema

Hata hivyo, Seong-beom amesema kuwa idadi ya waliofariki dunia inaweza kuongezeka.

Rais wa Korea Kusini Yoon Suk-yeol amewaagiza maofisa kupeleka timu za huduma ya kwanza na kuweka tayari vitanda hospitalini kwa ajili ya kuwahudumia walioathirika.