Ajali yaua mmoja, kujeruhi wanne Handeni

Muktasari:

  • Katika ajali hiyo mtoto wa miaka mitatu pia amejeruhiwa akiwa na wazazi wake.

Handeni. Mtu mmoja amefariki dunia na wengine wanne wamejeruhiwa katika ajali ya pikipiki iliyotokea eneo la Msasa wilayani Handeni mkoani Tanga.

  

Ajali hiyo imetokea jana Alhamisi Novemba 24, 2022 jioni ambapo pikipiki mbili zimegongona wakati moja ikiwa inakatisha barabara na nyingine kuigonga kwa nyuma.


Shuhuda wa ajali hiyo Ramadhani Lugenga amesema moja ya pikipiki ilibeba familia moja ambao ni baba, mama na mtoto wao wa miaka mitatu na hapa shuhuda wa ajali hiyo.


"Nilisikia watu wanapiga kelele nikafika eneo la tukio kufika ni ajali ya pikipiki na abiria wote wakiwa chini,ila mmoja ambae ni mkazi wa hapa hapa alifariki dunia hapa hapa eneo la tukio", amesema shuhuda huyo.


Mganga wa zamu Hospitali ya Mji Handeni, Edward Mhina amekiri kupokea mwili wa mtu mmoja na majeruhi wanne akiwemo mtoto mdogo wa miaka mitatu.


Amesema majeruhi hao wanaendelea kupatiwa matibabu ambapo wapo walioumia miguu, mikono na kuchubuka maeneo mbalimbali ya miili yao.


Akiwa hospitali hapo kusaidia majeruhi hao, Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji Handeni, Mussa Mkombati amesisitiza uvaaji kofia ngumu kwa abiria wakiwa kwenye usafiri wa pikipiki, kwani wengi hawafanyi hivyo.


Aliyefariki kwenye ajali hiyo ni mwananchi wa Msasa Anna Daud (74) na majeruhi ni Shabani Adamu, Dickson Mwankindi, Zawadi Kione na Sakina Juma.