Amlawiti mtoto wa mwaka mmoja kwa imani za kishirikina
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Wilbroad Mutafungwa
Muktasari:
Tukio hilo, limetokea Juni 21 saa tatu asubuhi katika kata ya Ndono.
Tabora. Kadege Thabit (18), mkazi wa Utemini wilaya ya Uyui mkoani hapa anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumlawiti mtoto wa mwaka mmoja na miezi miwili kutokana na imani za kishirikina.
Tukio hilo, limetokea Juni 21 saa tatu asubuhi katika kata ya Ndono.
Akizungumzia tukio hilo leo Juni 27, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Wilbroad Mutafungwa, amesema mtuhumiwa alimchukua mtoto huyo na kumwingilia kinyume cha maumbile.
Kamanda Mutafungwa ameeleza kwamba mtuhumiwa alitenda tendo hilo baada ya kumchukua mtoto huyo kutoka kwa mama yake akidai anaenda kumnunulia maandazi.
Ameongeza kuwa mtuhumiwa baada ya kumnunulia maandazi mtoto huyo alimpeleka chumbani kwake akafunga mlango ndipo akatenda unyama huo.
“Uchunguzi wa awali uliofanywa na Jeshi la polisi umebaini kuwa sababu za kufanya ukatili huo ni imani za kishirikina, na kwamba uchunguzi zaidi wa tukio hilo bado unafanyika,” amesema
Kamanda Mutafungwa amefafanua kwamba mtuhumiwa baada ya kukamatwa na kuhojiwa alidai kuwa alitenda kosa hilo kutokana na maelekezo ya mganga mmoja wa kienyeji kwamba ataweza kupata mali nyingi.