Baa ya La Chaaz yateketea kwa moto Dar
Muktasari:
Baa ya La Chaaz Lounge iliyopo Sinza Mori wilayani Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam imeteketea kwa moto leo jioni Ijumaa Machi 5, 2021.
Dar es Salaam. Baa ya La Chaaz Lounge iliyopo Sinza Mori wilayani Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam imeteketea kwa moto leo jioni Ijumaa Machi 5, 2021.
Baraka Bernard shuhuda wa tukio hilo amesema,” tulikuwa tukitazama mpira wa Simba Queens na Yanga Queens ghafla tukasikia watu wakisema kuna moto...,tulipotoka tukauona ulianzia kwenye ghala la kuhifadhia vinywaji kisha kusambaa maeneo mengine.”
Aman Abeid amesema moto huo ulianza kama masihara na ulisambaa kwa kasi katika maeneo mbalimbali ya ikiwemo kwenye fremu.
"Ghafla tuliona moshi ukitoka juu, kadri muda ulivyozidi kwenda moto ulikuwa ukisambaa kwa kasi. Eneo hili kulikuwa na sintofahamu watu walikimbia huku na kule ili kujiokoa hasa waliokuweko kwenye baa,” amesema Abeid.
Kaka wa mmiliki wa baa hiyo, Edwin Urio amesema, “tumepata hasara kubwa, imetokea kama hitilafu ya umeme ghafla tukasikia mlio kwenye dari kuangalia ndani ya dakika tano tukaona cheche. Tulihisi ni hitilafu ya umeme tukapiga simu gari la maji ambalo lilifika ndani ya dakika 20 na walipojaribu kuzima hawakufanikiwa maji yaliwahishia.”
"Moto ulizidi kuwaka kwa kasi hakuna tulichofanikiwa kuokoa tumepata hasara kubwa sana...,siwezi kusema ni kiasi gani kwa sasa hadi baadaye tutakapopiga mahesabu.”
Msimamizi wa kikosi cha Zimamoto na Uokoaji, Lyimo Shao amesema baada ya kupata taarifa walifika na kukuta moto mkubwa ukiwaka kwenye fremu na maeneo mengine.
"Ulikuwa moto mkubwa lakini tulifanikiwa kuudhibiti ili usiendelee maeneo mengine kwa sababu baa hii imekaribiana na makazi ya watu. Sehemu za mbele ya baa hii zimeathirika sana," amesema Shayo.