Chongolo awaonya makada wanaofitini wagombea ndani ya CCM

Muktasari:

  • Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo ameonya viongozi wanaoacha dhamana walizopewa na kukalia kueneza fitina na majungu dhidi ya wagombea wa nafasi za uongozi wakati huu wa uchaguzi wa chama hicho.

Shinyanga. Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo, amewaonya viongozi waliopewa dhamana na chama hicho, kuacha kueneza fitina na majungu dhidi ya wengine wakati wa uchaguzi wa ndani.

Chongolo ameyasema hayo leo Mei 27, 2022 wakati akisalimia wanachama wa CCM Mkoa wa Shinyanga, alipofika kwa ajili ya ziara ya kikazi.

Mtendaji Mkuu huyo wa CCM, amesema chama hicho kina utaratibu, Katiba, Kanuni na miongozo iliyondaliwa vizuri.

"Tatizo lililopo ni baadhi ya wanaopewa dhamana kwenye maeneo kutokutenda haki. Marufuku kwa yeyote kuineza fitina, majungu, uongo na uzushi dhidi ya wengine wakati wa uchaguzi," amesema.

Amewataka kutenda haki, akieleza kuwa haiwezekani wakati wote tangu mwaka 2017 viongozi hao wamekuwa ndani ya CCM lakini hawakuwahi kuonywa wala kujadiliwa kwenye vikao vya maadili, iweje tuhuma hizo ziibuke sasa.

"Kwenye kikao cha maadili haitwi, kwenye kikao cha kuulizwa haitwi, kwenye kikao cha kuhojiwa haitwi, mmefika wakati wa uchaguzi vikao asubuhi mchana jioni. Ooh... huyu mbaya, huyu mlevi, huyu mfupi, huyu mnene, anakuhusu nini?" amehoji.

Iwapo tuhuma hizo za kweli, amehoji kwanini hazikuibuliwa wakati mwingine na hatimaye waziibue kwenye uchaguzi.

Chongolo amesema huo ni ujanja ujanja wa kukata majina na kuzalisha viongozi wasio na sifa

Pia, ameagiza kuwekwa pembeni viongozi wa CCM wanaowania nafasi kwenye uchaguzi na badala yake wateuliwe wengine kushiriki vikao vya maamuzi dhidi ya wagombea wote.

"Kuanzia leo nchi nzima, mahali ambapo pana kiongozi anayegombea, kiongozi huyo atakaa pembeni asishiriki kikao cha maamuzi ili awatendee haki wenziwe na wenziwe wamtendee haki yeye," amesema.

Kinyume na kufanya hivyo, amesema ujanja ujanja wa kuficha fomu na kupitisha viongozi wasio na sifa hautaisha.

Katika hatua nyingine, Chongolo amesema ziara yake hiyo imelenga mambo matatu ambayo ni kuimarisha chama, kukagua miradi ya maendeleo na kuwasalimu wana-CCM.