Diamond aibukia kampeni za Raila Odinga

Mwanamuziki mashuhuri nchini Tanzania na Afrika Mashariki, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz akiwa kwenye mkutano wa kufunga kampeni za mgombea urais wa Kenya kwa tiketi ya Azimio la Umoja, Raila Odinga kwenye uwanja wa Kasarani. Picha na Francis Nderitu

Muktasari:

Mwanamuziki mashuhuri nchini Tanzania na Afrika Mashariki, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz leo ametumbuiza kwenye mkutano wa kufunga kampeni za mgombea urais wa Kenya kwa tiketi ya Azimio la Umoja, Raila Odinga kwenye uwanja wa Kasarani.

Nairobi. Mwanamuziki mashuhuri nchini Tanzania na Afrika Mashariki, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz leo ametumbuiza kwenye mkutano wa kufunga kampeni za mgombea urais wa Kenya kwa tiketi ya Azimio la Umoja, Raila Odinga kwenye uwanja wa Kasarani.

Msanii huyo amepanda jukwaani huku baadhi ya watu wakiwa na kumbukumbu ya habari zilizosambaa katika mitandao ya kijamii zikiwaonyesha baadhi ya wanafamilia wa msanii huyo wakiwa safarini kwenda nchini Afrika Kusini kwa ajili ya kushiriki sherehe ya kuzaliwa ya mtoto wa msanii huyo, Latifa Naseeb

Diamond alipandishwa jukwaani na mshehereshaji wa kampeni hizo na kuzusha shangwe nyingi kutoka kwa watu waliohudhuria kampeni hiyo kwenye uwanja huo unaoingiza watu 60,000.

Diamond ameimba nyimbo mbili jukwaani ambazo ni ‘baba lao’ na ‘Yope’ pia kabla ya kushuka alimnadi mgombea huyo na kumtakia kila la kheri kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Kenya utakaofanyika Jumanne, Agosti 9 mwaka huu.

Leo asubuhi msanii huyo alionekana kwenye video fupi iliyosambaa kwenye mitandao ya kijamii akitoka Afrika kusini na kuelekea Kenya pamoja na binti yake Latifa Naseeb.