Hai kufanya maombi siku saba kushukuru Mbowe kuachiwa huru
Mwehyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akitete jambo na mkewe, Dk Lilian Mbowewakati wa ibada ambayo imefanyika katika Usharika wa Nshara Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT). Picha na Janeth Joseph
Muktasari:
Mchungaji kiongozi Usharika wa Nshara Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kikutheri Tanzania (KKKT), Rodrick Mlay ametangaza maombi ya siku saba kwa ajili ya kumshukuru Mungu kuwezesha Mwehyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuachiwa huru.
Hai. Mchungaji kiongozi Usharika wa Nshara Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kikutheri Tanzania (KKKT), Rodrick Mlay ametangaza maombi ya siku saba kwa ajili ya kumshukuru Mungu kuwezesha Mwehyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuachiwa huru.
Mchungaji Mlay ameyasema hayo leo Jumapili Machi 20, 2022 wakati akizungumza kwenye ibada ya shukrani ya Mbowe na familia yake.
"Tutafanya maombi ya siku saba kuanzia kesho Jumatatu 12:00 jioni hadi saa 2:00 usiku, kuendelea kumshukuru Mungu kwa matendo yake makuu" amesema Mchungaji Mlay.
"Leo ni siku ya furaha kwa kuwa mwenzetu aliyekuwa kwenye mahangaiko amekuwa huru, tunaungana naye kumshukuru Mungu"
Ibada hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chadema ambao wamemsindikiza Mbowe kwenye shukrani, pia imehudhuriwa na wachungaji mbalimbali pamoja na Askofu mstaafu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Erasto Kweka.
Jana Mbowe aliwasili kijijini kwao Machame Wilaya ya Hai ambapo amesindikizwa na maelfu ya wananchi kutoka uwanja wa ndege wa KIA hadi zilipo ofisi za chama hicho, mji mdogo wa Bomang'ombe alipozungumza na wananchi na baadaye nyumbani kwake Machame.