Mbowe ashukuru polisi kuimarisha ulinzi mapokezi yake
Muktasari:
- Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amelishukuru Jeshi la polisi Mkoa wa Kilimanjaro kwa namna walivyoimarisha ulinzi wakati wa mapokezi yake wilaya ya Hai na kueleza “Hii ndio Tanzania tunayoitaka”
Hai. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amelishukuru Jeshi la polisi Mkoa wa Kilimanjaro kwa namna walivyoimarisha ulinzi wakati wa mapokezi yake wilaya ya Hai na kueleza “Hii ndio Tanzania tunayoitaka”
Wakati Mbowe akishuka uwanja wa Ndege Kia, ulinzi uliimarishwa na jeshi la polisi katika eneo la uwanja wa ndege, malango ya kuingia na kutoka uwanjani humo pamoja na barabarani alikopita ambapo askari walionekana kuongoza msafara huo.
Msafara huo ukitoka KIA, wafuasi wa chama hicho walitembea kwa miguu wakilisukuma gari la Mbowe hadi Bomang'ombe zilipo ofisi za chama hicho, huku magari yakilazimika kwenda mwendo wa pole, hali iliyosababisha shughuli za barabara kusimama kwa muda.
Mbowe ameyasema hayo leo Jumamosi Machi 19,2022 wakati akizungumza na wananchi waliokuwa wamekusanyika katika ofisi ya chama hicho Bomang'ombe Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro.
“Jaribu kufikiria leo nimepokelewa Kilimanjaro (Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro) askari polisi walikuwepo hajapigwa mtu bomu, hajakanyagwa sisimizi, hajaumizwa mtu yoyote, polisi asanteni sanaa, hii ndio Tanzania tunayoitaka “ amesema Mbowe
Katika mapokezi hayo Mbowe amepewa zawadi mbalimbali ikiwemo Ng'ombe sita na mbuzi zaidi ya 10.