Mgombea wa ACT Wazalendo atoka nje ya ukumbi asisikilize matokeo akidai hana imani nayo

Pemba. Mgombea ubunge wa Jimbo la Konde kupitia ACT Wazalendo, Mohamed Said Issa ametoka ndani ya ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Micheweni yanapofanyika majumuisho ya uchaguzi akidai kutokuwa na imani na kitakachotangazwa.

Amefikia hatua hiyo baada ya msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo, Yassin Khamis kueleza kwamba kinachofanyika sasa ni kuweka matokeo hayo kwanza kwenye mfumo kabla ya kutangaza mshindi

Ndipo Issa aliamka na kueleza dukuduku lake akisema katika baadhi ya vituo mawakala wake hawakusaini matokeo ya uchaguzi kutokana na taratibu zilizokiukwa

"Mheshimiwa mimi sina imani na matokeo haya, kwasababu mawakala wangu hawakuyasaini kwenye vituo walinyimwa fomu kwahiyo mimi sina sababu ya kuendelea kukaa humu maana siwezi kuamini kinachofanyika hapa," amesema na kuondoka nje

Hata hivyo kabla hajatoka nje, msimamizi wa uchaguzi amemueleza kuwa vituo anavyolalamikia wakala wake kutosaini lakini karatasi zinaonyesha zimesainiwa na mawakala wake.

Hata hivyo Issa aliendelea kupinga mawakala wake kusaini karatasi hizo akidai kama zitakuwa zimesainiwa basi wamesaini watu wengine ambao hawawatambui.