Miradi ya Sh65.3 bilioni yakataliwa na Mwenge wa Uhuru

Miradi ya Sh15.3 bilioni yakataliwa na Mwenge wa Uhuru

Muktasari:

  • Jumla ya miradi 49 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Sh65.3 bilioni imekataliwa na kiongozi wa mbio ya Mwenge wa Uhuru 2021 baada ya kutiliwa shaka.


Chato. Jumla ya miradi 49 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Sh65.3 bilioni imekataliwa na kiongozi wa mbio ya Mwenge wa Uhuru 2021 baada ya kutiliwa shaka.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Jenista Mhagama amesema miradi hiyo iko katika wilaya 38 katika ya wilaya 150 zilizotembelewa na mbio za Mwenge mwaka huu.

Akitoa taarifa ya shughuli za Mwenge wa Uhuru wakati wa kilele cha mbio hizo zinazofanyika Chato leo Oktoba 14, Waziri Mhagama amesema tayari Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imefanya ukaguzi na matokeo yatawasilishwa kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi na hatua zaidi.

"Miradi yote iliyotiliwa mashaka ya kuwepo vitendo vya ubadhirifu haikuzinduliwa wala kuwekewa mawe ya msingi kwa sababu viongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru hawakuta kujihusisha nayo na waliagiza Takukuru kufanya uchunguzi," amesema Waziri Mhagama

Ameongeza; "Taarifa ya uchunguzi wa miradi hii itawasilishwa kwako mheshimiwa Rais leo leo kwa uamuzi na maelekezo ambayo sisi tuko tayari kuyatekeleza,"

Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizozinduliwa Mei 17 zinahitimishwa leo wilayani Chato zikiambatana na maadhimisho ya miaka 22 ya kifo cha Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.

Hadi zinahitimishwa leo, Mwenge wa Uhuru umekimbizwa umbali wa kilometa 21, 480. 16 ukipita wikaya 150.

Mwenge huo wa Uhuru umetembelea, kukagua, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi 1, 067 yenye thamani ya zaidi ya Sh1.2 trilioni.

Miradi hiyo ni kutoka sekta za maji, nishati, afya, kilimo, uvuvi, mifugo na  miundombinu.