Mwanafunzi wa darasa la kwanza aliwa na mamba Sengerema
Muktasari:
- Wananchi wa Kata ya Maisome wameiomba Serikali kuwachimbia visima ili kuwaepusha na matukio ya kuliwa na mamba yanayogharimu maisha ya watu.
Buchosa. Janeti Mganga (8) aliyekuwa anasoma darasa la kwanza shule ya msingi Busikimbili iliyoko kata ya Maisome, Halmashauri ya Buchosa, wilayani Sengerema mkoani Mwanza ameuawa na mamba wakati akioga kwenye Ziwa Victoria huku baadhi ya viungo vya mwili wake vikiwa vimenyofolewa na kutafunwa na mamba huyo.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Emmanuel Kipole, amesema mwanafunzi huyo alikutwa na tukio hilo wakati alipokua akioga na wanafunzi wenzake katika Ziwa Victoria.
Kipole amewasihi wazazi wasiwaruhusu watoto wao kwenda kuogelea ziwani badala yake wateke maji na kwenda majumbani.
"Nitumie nafasi hii kuwaomba wananchi wajiepushe kuogea ziwani, na wasiwaruhusu watoto wao kwenda kuogea au kuchezea ziwani," alionya Kipole.
Naye Diwani wa Kata ya Maisome, Dauson Miyaga amechukizwa na visa vya mamba kuendelea kugharimu maisha ya watu na kuzitaka mamlaka husika kuchukuwa hatua juu ya mamba hao.
" Nimelalamika mara kwa mara kwa mamlaka husika lakini hazichukui hatua zozote naomba zitusaidie," amesema Miyaga.
Wakati Ofisa mtendaji Kijiji cha Busikimbi, Salimu Magayi amesema wamesikitishwa na kifo hicho na kueleza huenda mwanafunzi huyo pengine angekuwa kiongozi katika siku za usoni.
Amewaomba wananchi wawe wavumilivu kwani wao wapo kwa ajili ya kusaidia wananchi ikiwemo kutatua kero zilizopo katika jamii.
Wakati Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Busikimbi, Kosmas Makoye alithibitisha tukio la mwanafunzi kuliwa na mamba.
"Tumelipokea kwa mshituko mkubwa ila tunaomba serikali yetu itujengee visima vya maji ili kupunguza mlundikano wa watu kwenda kuogea ziwani," amesema Makoye.
Wiribeti Mangapera, ambaye ni mkazi wa Kata ya Maisome ameeleza kuwa visa vya mamba kula watu vimekuwa vikiongezeka kila siku na hivi karibuni walimpoteza Raulensia Igayo, ambaye ni mkazi wa kijiji cha Kisaba ambacho ni kijiji jirani na Busikimbi.