Ndugai ataka mgawanyo wa miradi ufuate idadi ya watu

Ndugai ataka mgawanyo wa miradi ufuate idadi ya watu

Muktasari:

  • Spika wa Bunge Job Ndugai, ameshauri mgawanyo wa miradi inayotokana na Sh1.3 trilioni zilizotolewa na Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) ufuate idadi ya watu na si jimbo na zikibaki zipelekwe kwenye sekta ya kilimo.

Dodoma. Spika wa Bunge Job Ndugai, ameshauri mgawanyo wa miradi inayotokana na Sh1.3 trilioni zilizotolewa na Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) ufuate idadi ya watu na si jimbo na zikibaki zipelekwe kwenye sekta ya kilimo.

Kauli hiyo ameitoa leo, Jumapili Oktoba 10, 2021 katika uzinduzi wa kampeni ya maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya Uviko-19 baada Waziri wa Fedha na Mipango Dk Mwigulu Nchemba kusema kuwa kutokana na fedha hizo kila jimbo litapata madarasa mapya 70.

Spika Ndugai amesema kuna majimbo mengine yana idadi kubwa ya watu na kata hivyo kugawa fedha hizo kwa majimbo sio haki.

Ametoa mfano kuwa halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa ina majimbo mawili kwa hiyo itapata madarasa 140 lakini Wilaya ya Kongwa ambayo ina jimbo moja ya uchaguzi itapata madarasa 70 tu.

Spika Ndugai amesema fedha hizo zimefuata taratibu kwa Bunge kupanga matumizi yake wakishirikiana na maofisa wa waandamizi wa Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Waziri mhusika.

Amesema kuwa Kamati ya Bunge ya Bajeti kwa niaba ya Bunge wametoa mapendekezo na anaamini kuwa Wizara ya Fedha na Mipango itazingatia.

Amesema wamefanya hivyo kwasababu wasingeweza kusubiri hadi mkutano unaoanza Novemba 2 mwaka huu kwasababu utekelezaji wa miradi hiyo unatakiwa kumalizika kabla ya Juni mwakani.