NFRA yaanza ununuzi mazao

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma kuhusu maandalizi ya kuanza ununuzi wa mazao yatakayovunwa msimu huu wa kilimo yatakayoanza kesho. Picha na shakila Nyerere

Muktasari:

Serikali imesema kuanzia kesho Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) itafungua vituo vyake na kujiandaa kuingia sokoni kwa ajili ya kununua mazao yatakayovunwa msimu huu.

Dodoma. Serikali imesema kuanzia kesho Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) itafungua vituo vyake na kujiandaa kuingia sokoni kwa ajili ya kununua mazao yatakayovunwa msimu huu.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumatatu Mei 23, 2022 na Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma akisema lengo ni kuhifadhi tani 100,000 za mahindi kwa msimu huu.

Bashe amesema kuwa miaka ya nyuma Wizara kupitia NFRA ilikuwa inachelewa kuingia sokoni ambapo mazao mengi yanakuwa yamesha nunuliwa na wanunuzi wa biashara hivyo imeona msimu huu ijiandae mapema.

Waziri Bashe amesema Wizara ya Kilimo imepitishiwa bajeti na Bunge ambapo kila mwaka wizara baada ya kupitishwa bajeti unapofika msimu wa mavuno hununua chakula na kuhifadhi. Amesema lengo la kununua tani 100,000 za mahindi ni kuwafanya wakulima kuendelea kujitanua katika soko la chakula ambapo Serikali haitoweza kufunga mipaka ya nchi kwa sababu itasababisha wakulima kukosa kufanya biashara na wageni.

Hata hivyo Waziri Bashe amesema kutokufunga mipaka ni kutokana na Serikali kutoweza kununua tani milion tano za mazao yaliyozalishwa na kusababisha kuporomoka kwa biashara ya chakula.

“Wizara imefanya uchunguzi wa uzalishaji wa chakula na kujiridhisha Serikali haitofunga mipaka kutokana na wakulima wamenunua bidhaa kwa bei kubwa, lakini hata Serikali haitokuwa na uwezo wa kununua tani 5 milion tano hivyo itasababisha kuporomoka kwa biashara ya kilimo” amesma Bashe

Amewashauri wakulima wanapouza chakula wakumbuke kuhifadhi chakula kutokana na msimu wa mwaka huu kuwa tofauti na kipindi kilichopita.