Ofisa wa polisi aeleza sababu ya kujijengea kaburi

Muktasari:

  • Patrick Matey Kimaro(59) maarufu Sabasita ambaye ni Mrakibu wa  Jeshi la Polisi nchini Tanzania amejijengea kaburi lake mwenyewe akitaka familia yake isihangaike siku ya mazishi yake.



Hai. Patrick Matey Kimaro(59) maarufu Sabasita ambaye ni Mrakibu wa  Jeshi la Polisi nchini Tanzania amejijengea kaburi lake mwenyewe akitaka familia yake isihangaike siku ya mazishi yake.

Mwananchi digital lilifika nyumbani kwake leo Ijumaa Januari 21,2022  katika kijiji cha Mbosho ,wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro na kushuhudia kaburi hilo.

Amesema mawazo ya kujenga kaburi lake  akiwa hai ni maamuzi yake binafsi na kwamba hakutaka familia yake ihangaike siku ya mazishi yake.

Amesema ilichukua muda kuieleza familia yake juu ya kujenga kaburi lake.

Akizungumzia  jeneza lake  amesema  atafanya utaratibu lakini hawezi kununua kwa sasa, “sio sasa kwa kuwa utengenezaji wa majeneza kwa wakati huo utakuwa na usasa wake”

Hata hivyo amewataka watanzania kumwelewa maamuzi aliyofanya kwani sio jambo baya na wala hajavunja sheria za nchi na kwamba kila binadamu atakufa.