Rais Mwinyi afanya mabadiliko Baraza la Mapinduzi
Mudrick Ramadhan Soraga aliyeuliwa kuwa Waziri Utalii na Mambo ya Kale akichukua nafasi ya Simai Mohamed Said aliyejiuzulu.
Muktasari:
- Mabadiliko hayo yamekuja ikiwa ni siku moja tangu aliyekuwa Waziri Utalii na Mambo ya Kale Simai Mohamed Said akijiuzulu jana.
Unguja. Rais wa Zanzibar Dk Hussein Mwinyi amefanya mabadiliko ya baraza la Mapinduzi akiteua mawaziri wawili na kumbadilisha mmoja.
Katika mabadiliko hayo, Rais Mwinyi pia ameteua manaibu mawaziri wawili.
Taarifa iliyotolewa leo Januari 27, 2024 na Katibu Mkuu Kiongozi Zena Said imesema, Mudrick Ramadhan Soraga ameteuliwa kuwa Waziri Utalii na Mambo ya Kale akichukua nafasi ya Simai Mohamed Said aliyejiuzulu jana.
Kabla ya uteuzi huo Soraga alikuwa Waziri wa Uchumi, kazi na Uwekezaji
Rais Mwinyi pia amemteua Ali Suleiman Mrembo aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango kuwa Waziri Ofisi ya Rais Ikulu, huku aliyekuwa Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini, Ali Othman akiteuliwa kuwa Waziri Uchumi wa Buluu na Uvuvi na aliyekuwa Naibu Waziri wa Ardh, Juma Makungu Juma ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango.
Naye Salha Mohamed Mwinjuma ambaye ni Mwakilishi viti maalumu kundi la vijana ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Ardhi.
Mwingine ni Mwakilishi Konde Zawadi Nassor ambaye ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa maji, Nishati na Madini.
“Uteuzi huo unaanza Leo Januari 27, 2024.” imesema taarifa hiyo.