Sababu kuu za upungufu nguvu za kiume hizi hapa

Muktasari:

Daktari bingwa wa upasuaji wa tumbo na kifua wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Maurice Mavura anasema tatizo la ukosefu wa nguvu za kiume lipo.

Pombe, maradhi na ulaji wa vyakula usiozingatia maoni ya wataalamu wa afya na tiba lishe ni baadhi ya mambo yanayotajwa kusababisha upungufu wa nguvu za kiume.

Tatizo la upungufu wa nguvu za kiume linatajwa kushika kasi na limesababisha baadhi ya wanaume kadhaa kuishi maisha ya uyonge yaliyojaa hofu hasa kuhusu hatima ya uhusiano wa ndoa zao.

Kutokana na hali hiyo, baadhi ya waathirika hao wameendelea kuhangaika kurejesha heshima kwenye ndoa zao kwa kusaka tiba, wengine hospitali na wengine kwa waganga wa jadi.

Daktari bingwa wa upasuaji wa tumbo na kifua wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Maurice Mavura anasema tatizo la ukosefu wa nguvu za kiume lipo.

“Haya matatizo yalikuwapo, isipokuwa inaonyesha wengine waliougua tatizo hilo waliogopa kwenda hospitali kusaka tiba,” anasema Dk Mavura.

Anasema: “Pengine walishindwa kujitokeza kwa kuhofia unyanyapaa au kuona aibu, lakini kwa sasa wengi wao uoga umewatoka wanafika kutibiwa matatizo hayo ikiwamo tezi dume,”anasema.

Dk Mavura anasema kutokana na sababu hizo, ni vigumu kueleza idadi ya wenye matizo ya nguvu za kiume kama wameongezeka ama wanapungua.

“Lakini pia kwa watu sasa kujitokeza na kuja kutibiwa huenda uelewa umeongezeka baada ya kupata elimu na sasa wameona umuhimu wa matibabu,”anasema Dk Mavura.

Matibabu

Anasema wanatibu matatizo hayo kwa njia mbalimbali, lakini upasuaji wa kuweka vipandikizi vya mirija kwenye uume bado hawajaanza kuufanya nchini, licha ya kufanyika katika hospitali zingine za nje ya nchi.

“Upasuaji huo kuna baadhi ya nchi zenye vifaa hivyo zinafanya, hapa kwetu bado hatujaanza,” anasema Dk Mavura.

Daktari Anna Sarra wa Muhimbili anasema tatizo hilo ambalo kitaalamu linanaitwa Ericticle Dysfunction husababisha na mambo mengi ikiwamo maradhi.

Anayataja maradhi hayo ni pamoja na kisukari, shinikizo la damu (BP), uti wa mgongo (Spinal cord) na kuharibika kwa mishipa kutokana na upasuaji.

Dk Sarra anasema ili mwanaume amudu kushiriki tendo la ndoa, anatakiwa mfumo wake wa damu uwe kwenye mzunguko unaotakiwa, pia ubongo, mishipa ya fahamu na homoni.

“Kutokana na kuugua maradhi niliyotaja, pia kuna dawa zinazochangia kupunguza nguvu za kiume. Zipo ambazo husababisha homoni kushindwa kuwa katika mfumo wake wa kawaida, hivyo kumletea athari mwanaume,” anasema na kuongeza:

“Pia, kuna baadhi ya miili ya watu inatambua sukari kama adui, hivyo husababisha kuchomwa sindano ya DM I, kwa kawaida hupatwa na ganzi, wengine hupatwa matatizo ya kisaikolojia, hivyo hupoteza hisia za mapenzi,” anasema Dk Sarra.

Mtindo wa maisha unavyomuathiri mwanaume

Dk Sarra anasema mtindo wa maisha wa baadhi ya wanaume, ikiwamo unywaji wa pombe kupita kiasi, uvuta sigara na dawa za kulevya aina zote huchangia tatizo la upungufu wa nguvu za kiume.

Anasema mtindo wa ulaji wa vyakula bila kuzingatia ushauri wa wataalamu wa afya na tiba lishe, hasa ulaji wa nyama nyekundu, ni miongoni mwa sababu zinazochangia upungufu wa nguvu za kiume.

Wanaume wenye umri gani wako hatarini zaidi

Dk huyo anasema wanaume wenye umri kati ya miaka 40 na kuendelea ndiyo hukumbwa na tatizo hilo.

Hata hivyo, anasema wapo wengine ambao si wengi sana wenye umri chini ya miaka 40 hukumbwa na tatizo hilo.

Dk Sarra anasema tatizo hilo linaweza kutibiwa kama mtu atakubali kufanyiwa uchunguzi na wataalamu.

Anasema matatizo ya nguvu za kiume yanatibika kwa njia mbalimbali, ikiwamo mhusika kutibiwa kwa dawa aina ya Viagra.

“Viagra inatibu tatizo hilo kwa vipimo maalumu vinavyotolewa na daktari, lakini wapo ambao wamebaini hiyo ni dawa, huamua kuitumia bila maelekezo ya daktari na hujikuta wakipata matatizo zaidi,” anasema Dk Sarra.

Njia nyingine ya kutibu tatizo hilo ni kwa muathirika kufanya mazoezi ya kutosha.

Anasema matibabu hayo huwaelekeza waathirika kuyafanya kwa ratiba maalumu.

“Mazoezi ni muhimu na ni tiba nzuri kwa sababu husaidia kufanya mzunguo wa damu kwenda vizuri mwilini hali inayoisaidia mishipa ya viungo kufanya kazi inavyotakiwa,” anasema Dk Sarra.

Waganga wa tiba asili nao walonga

Tabibu wa tiba za asili, Omari Kuyunguyo wa Jijini Dar es Salaam anasema tatizo la nguvu za kiume linawakumba wanaume wengi hivi sasa tofauti na miaka 15 iliyopita ambayo amekuwa akiifanya kazi hiyo.

“Huu ni mwaka wangu wa 16 nafanya kazi ya kutibu, hapa sina daftari lakini nakuhakikishia, wanaume wengi wanaofika kwangu kusaka tiba ya tatizo la nguvu za kiume ni wengi,” anasema Kuyunguyo.

Anasema kati ya wanaume 100 wakiwamo vijana wanaofika kutibiwa kwake kwa mwezi, 80 wanakabiliwa na tatizo la upungufu wa nguvu za kiume.

“Sababu za kuugua zipo tofauti, lakini wanaume wengi wanaugua tatizo hilo na mimi nimewahi kuugua,” anasema Kuyunguyo na kuongeza:

Tabibu mwingine, Sheikh Swalehe Kayumbo wa Tanga anasema amefanya shughuli hiyo kwa miaka 45, lakini ni jambo la kushangaza kuona wanaume wengi wanaofika kwake wanasumbuliwa na upungufu wa nguvu za kiume.

“Hasa waishio mjini kwa sababu wengi wanakula vyakula vya kukaanga na kukoboa, pia hata viungu vinavyotumika kwenye mboga vingi vina kemikali, mfano ndimu ya unga huwezi kufananisha na ile ya tunda, matokeo yake ndiyo hayo wanaume wengi wanajikuta wanashindwa kutomiza wajibu wao,” anasema.

Kayumbo anabainisha kuwa gharama za tiba anazotoza ni kuanzia Sh50,000 ingawa pia inaweza kupanda kulingana na ukubwa wa tatizo.

“Tatizo hili linaweza kuepukwa kwa wanaume kujikita kula vyakula vya asili ikiwamo asali na maziwa ya ng’ombe halisi kila siku,” anasema.

Anasema wakipenda chipsi na nyama choma hasa kuku wa kisasa ambao wengi hula na kutafuta hadi mifupa, wajiandae kubeba gharama za matibabu.