Samia ateua makatibu wakuu

Samia ateua makatibu wakuu

Muktasari:

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Jumapili Aprili 4, 2021 amefanya uteuzi wa makatibu wakuu wa wizara, naibu makatibu wakuu na wakuu wa taasisi mbalimbali huku baadhi wakihamishwa.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Jumapili Aprili 4, 2021 amefanya uteuzi wa makatibu wakuu wa wizara, naibu makatibu wakuu na wakuu wa taasisi mbalimbali huku baadhi wakihamishwa.
Katika uteuzi huo aliyekuwa katibu mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dotto James amehamishiwa kuwa katibu mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara.

Dk Hassan Abbas amebaki kuwa katibu mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo huku nafasi yake ya msemaji mkuu wa Serikali akiteuliwa aliyekuwa mkurugenzi wa mawasiliano ya rais Ikulu, Gerson Msigwa.

Katika mabadiliko hayo, Rais Samia amewaondoa waliokuwa wakuu wa taasisi mbalimbali za Serikali akiwemo mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Deusdedit Kakoko ambaye amesimamishwa kupisha uchunguzi, sasa nafasi yake ameteuliwa Erick Hamis.
Kiongozi mkuu huyo wa nchi pia ameigusa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) baada ya kumteua Alhayo Kidata kuwa mkurugenzi wa mamlaka hiyo kuchukua nafasi ya Edwin Mhede huku Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) akiteuliwa Dk Jabir Kuwe anayechukua nafasi ya James Kilaba.