Simbachawene awaonya manabii, mitume

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imewaonya manabii na mitume ambao hawako katika mwamvuli wa taasisi huku ikiwataka pia wasiochukua vitambulisho vyao vya Taifa kujitokeza kuvichukua

Dodoma. Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Tanzania, George Simbachawene amewaonya manabii na mitume kuacha kutoa huduma hizo kama hawako chini ya taasisi iliyosajiliwa na Serikali na watakaokaidi wasije wakalalamika kwa yatakayowakuta.

Simbachawene ameyasema hayo leo Ijumaa Novemba 26, 2021 wakati akizungumza kuhusu mafanikio ya Wizara ya Mambo ya Ndani katika miaka 60 ya uhuru wa Tanzania Bara,

Simbachawene amesema hakuna sheria inayosimamia mitume na manabii na kwamba hakuna huduma ya mtu mmoja kama inavyodaiwa kuanzishwa na wahubiri hao.

“Sisdi kwa mujibu wa sheria za nchi ni hadi inapokuwa jumuiya ya watu kadhaa ndipo tunaposema kiongozi wake anaitwa fulani lakini mtu mmoja anatembea kutoa huduma kwenye nyumba za watu yakikukuta usije kutulalamikia,”amesema

Amesema wapo baadhi ya watu wanatumia unabii na mitume katika kuwadhulumu mali ama kuwaibia watu na kuwataka watanzania kujiadhari nao.

“Watu wengi wameumia, hakuna sheria ya kukusaidia mlikopeana kama mlipeana zawadi. Ukisema amekuibia yeye anasema ulitoa sadaka,”amesema.

Amesema wanaendelea kupambana nalo hilo lakini watu waende kusali katika taasisi zenye watu zinazoeleweka.

Amewataka manabii na mitume kwenda katika mwamvuli wa taasisi inayoeleweka ili kunapotokea jambo Serikali ifahamu mahali pakufuatilia.

Aidha, Simbachawene amewataka watu kujitokeza kuchukua vitambulisho vyao vya Taifa ambavyo viko tayari katika ofisi za Mamlaka ya Vitambulisho Nchini (Nida).

Simbachawene amesema kuwa hadi sasa kuna jumla ya vitambulisho milioni 1.1 kati ya vitamvulisho vilivyozalishwa na kusambazwa sehemu mbalimbali wilayani bado havijachukuliwa na wenyewe.

Amesema miongoni mwap ni vitambulisho 206,959 ambavyo viko katika ofisi za usajili za wilaya na 896,863 vipo katika ofisi za Serikali za kata na vijiji/mitaa katika mikoa 31 ya Tanzania Bara na vIsiwani.

Simbachawene ametaka mamlaka hiyo kutangaza orodha ya watu wenye vitambulisho hivyo kwenye vyombo vya habari ili wenyewe wakavichukue.