Swahili Fashion Week yazinduliwa jijini Dar
Muktasari:
Swahili Fashion yazinduliwa, mwaka huu video na filamu yenye ubunifu wa mavazi kupewa tuzo
Dar es Salaam. Onyesho la 13 la mitindo almaarufu kama Swahili Fashion Week limezinduliwa leo likitarajiwa kuufanyika kwa siku tatu na kuwahusisha wabunifu 45 kutoka ndani na nje ya Tanzania.
Mwasisi wa onyesho hilo, Mustafa Hassanali amesema mwaka huu zitatolewa tuzo kwa wabunifu watakaofan ya vizuri kama ilivyo kawaida zikiwamo mbili mpya za mavazi ya kwenye filamu na video za muziki.
Mustafa amesema onyesho la mwaka huu linafanyika katika kipindi ambacho Tanzania na dunia inapambana na virusi vya corona vilivyoteteresha uchumi.
“Ni mwaka wa changamoto, hatukutegemea kama onyesho lingefanyika kutokana na hali ya uchumi na namna ambavyo wabunifu wamepitia wakati mgumu,” amesema Hassanali.
Mwaka huu amesema kutakuwa na mbunifu wa kimataifa kutoka Italia watakaotoa uzoefu wa ziada kwa Watanzania kujifunza.
Kwa upande wake, katibu mtendaji wa Baraza la Sanaa Tanzania (Basata), Geofrey Mngereza amesema jukwaa hilo ni muhimu kwa wabunifu na wasanii nchini pamoja na Taifa kwa ujumla.
Amesema maendeleo ya viwanda yanategemea wabunifu ndiyo maana Serikali iko pamoja na wadau wa sekta hiyo.
“Tumeona mchango mkubwa ambao wabunifu wameuonyesha wakati wa corona kwa kutengeneza barakoa kwa kutumia malighafi zinazopatika nchini. Tuendelee kuwaunga mkono na itapendeza kama Watanzania wataona tija ya kutumia bidhaa yakiwamo mavazi,” amesema Mngereza.