Takukuru yasaini makubalino na wadhibiti dawa za kulevya
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Salum Hamduni
Dodoma. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na dawa za kulevya leo wameingia mkabata wa kufanya kazi pamoja kwa madai shughuli zao zinashabihiana.
Wakuu wa taasisi hizo leo Ijumaa Mei 26, 2023 wamesaidia memorandum hiyo jijini Dodoma wakisema kuwa, gari imewashwa na safari ya mapambano imepewa wenyewe.
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Salum Hamduni na Kamishina Jenerali wa Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo wamesaini mkataba huo wakieleza kwamba unalenga kuibadili Tanzania.
Akizungumza baada ya kusaini mkataba huo, Hamduni amesema wameingia makubalino ya kikazi ili kuongeza ufanisi katika mapambano ya rushwa na dawa za kulevya kwani makosa yake yanashabihiana.
Hamduni amesema rushwa ni kichocheo kikubwa kwenye dawa za kulevya hivyo wameamua kusimama pamoja ili kusukuma mapambano hayo.
Amesema mkataba huo utasaidia kuongeza nguvu kubwa na kwamba hakutakuwa na eneo la mharifu kupenya kwa kiburi cha fedha kama ambavyo ilikuwa ikitokea kwa baadhi ya wachache.
“Katika hili, tumeamua kwa pamoja kwamba tuanze na utoaji wa elimu kwa watumishi wetu ili kuwajengea uwezo wa kufanya kazi kwa pamoja na matokeo tutayaona kwani tumebaini kuwa inawezekana,” amesema Hamduni.
Kwa upande wake Kamishina wa Kupambana na dawa za kulevya Aretas Lyimo amesema rushwa na dawa za kulevya ni makosa ya kupangwa ambayo yakiwekewa nguvu ya pamoja hakuna kinachoshindikana.
Lyimo alisema wanakoelekea mambo yatakuwa mazuri na kupata Tanzania yenye uzalendo na wazalendo ndani ya Taifa.
Hata hivyo amesema kuwa wamejifunza kutoka Takukuru ambao wenzao wameanzia ngazi ya chini mashuleni hivyo na wao wa dawa za kulevya wanakwenda huko kwani kila makosa yameonyesha chanzo chake ni vijana.