VIDEO: Mikutano ya hadhara ya kisiasa ruksa Tanzania

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameruhusu mikutano ya hadhara ikiwa ni miongoni mwa agenda za muda mrefu vyama vya upinzani kutaka mikutano hiyo iruhusiwe.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameruhusu mikutano ya hadhara iiliyokuwa ikililiwa kwa muda mrefu na vyama vya upinzani kutaka ruhusiwe.

 Leo Jumanne, Januari 3, 2023  Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Samia amesema; "uwepo wangu leo hapa mahali nimekuja  kufanya ruhusa ya mikutano hii, nimekuja kutangaza kuondoa zuio la kuzuia mikutano ya hadhara na ninasema kwamba, sasa linaondoka."

Rais Samia amesema mikutano hiyo kisheria, ni haki haki kwa vyama vya siasa kuiendesha huku akisema kwa upande wa Serikali wamejipanga kutekeleza wajibu wao wa kulinda mikutano hiyo.

Ili kuendelea na mikutano hiyo, Rais Samia amesema jukumu sasa linabaki kwa vyama vya siasa kutoa taarifa kwa vyombo vya dola kama sheria na kanuni zinavyoelekeza ili vipatiwe ulinzi.

Rais amesema hatua waliyoifikia katika mazungumzo baina ya vyama hivyo na Serikali kwa sasa, mikutano hiyo haitazuiliwa tena.

"Ruhusa ya mikutano ya kisiasa itatolewa, wajibu wetu sisi Serikali ni kuwalinda mfanye mikutano yenu salama mmalize vizuri, kufuata kanuni ndio wajibu wenu vyama vya siasa," amesema.

Ikumbukwe kuwa hatua hiyo ya Rais Samia inakuja ikiwa ni takribani mwezi mmoja umepita tangu akabidhiwa ripoti ya kikosi kazi cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi, ambapo katika ripoti hiyo, viongozi wa vyama vya siasa waliweka bayana hitaji namba moja kuwa ni mikutano ya hadhara ambayo ilizuiliwa.

#LIVE: Rais Samia na viongozi wa kisiasa

Akiwasilisha mapendekezo ya kikosi kazi mwezi uliopita kwa Rais Samia, Mwenyekiti wa Kikosi Kazi hicho, Profesa Rwekaza Mukandala alisema kuwa kilipendekeza mikutano ya hadhara iruhusiwe kufanyika kwa mujibu wa katiba na sheria.

“Yafanyike marekebisho ya sheria ili kuhakikisha mikutano ya hadhara inafanyika kwa ufanisi, sheria hizo ni pamoja na Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258, Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi Sura 322, Kanuni za Maadili ya Vyama vya Siasa za mwaka 2019,” alisema Profesa Mukandala.

Leo akizungumza na viongozi wa vyama vya siasa, Rais Samia amesema atazungumza na vyombo vya dola ili kuhakikisha suala hilo linatekelezwa kwa ufanisi.

“Ni haki kwa vyama vya siasa kuendesha mikutano ya hadhara lakini ndugu zangu tuna wajibu. Kwa upande wa serikali tumeshajipa wajibu wetu kuwa ni kulinda mikutano ya vyama vya siasa, wajibu wenu vyama vya siasa ni kutupa taarifa kama sheria na kanuni zinavyosema kisha vyombo vinatoa ruhusa,” amesema

“Wakiona kuna hatari hawatoi ruhusa kwa hatua tuliyofika ruhusa za kufanya mikutano zitatolewa kwa sababu wajibu wetu ni kuwalinda mfanye mikutano kwa usalama, mmalize vizuri muondoke vizuri.”

Pia, amesema, “mimi siwaiti nyie vyama vya upinzani, vyama vya kuwaonyesha changamoto zilipo, mnapinga nini, mnampinga nani, ndani ya Tanzania tunapingana kwei, tunaonyeshana changamoto ziko wapi, kasoro ziko wapi na mkinionyesha nikiwa msikivu nikazitekeleza nitaongeza imani kwa wananchi.”

Rais Samia ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM amesema; “mazungumzo baina ya Serikali na vyama vya siasa bado yanaendelea, kuna mambo mengi ambayo itabidi tuitane, tuzungumze, tushauriwe, tukubali, tukatae kwa hoja lakini hivyo mazungumzo na maridhiano bado yanaendelea.”

“Mimi imani yangu, vyama vya siasa tutaendelea kukaa tuzungumze mambo yanayohisu nchi yetu,” amesema