Wakristo watakiwa kujenga utamaduni wa uvumilivu

Waumini wa dini ya Kikristo wakiwa kanisani. Picha Maktaba

Muktasari:

  •  Waumini wa dini ya Kikristo duniani kote wamejitokeza usiku wa kuamkia leo kushiriki ibaada ya kumbukumbu ya kuzaliwa Yesu Kristo miaka zaidi ya 2,000 iliyopita kwa ajili ya kuukomboa ulimwengu.

Dar es Salaam. Waumini wa dini ya Kikristo wametakiwa kuenzi utamaduni wa kumsifu Mungu wanapoadhimisha kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Bwana yesu Kristo miaka 2000 iliyopita.

Mbali na hilo, Wakristo pia wametakiwa kuwa na upendo na kujifunza kwa Wakristo wa mataifa mengine kuwa wavumilivu.

Hayo yameelezwa usiku wa kuamkia leo Desemba 25, 2023 katika ibada ya mkesha wa Krismasi iliyoongozwa na Msaidizi wa Askofu katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Azania Front Jijini Dar es Salaam Chediel Lwiza.

 “Yako mambo makubwa matatu nataka leo tuondoke nayo na ninaamini yatatusaidia tunapotafakari kuzaliwa kwa mwokozi wetu Yesu Kristo,” amesema.  

Katika mafundisho yake, Lwiza ametumia msingi wa Injili ya Mathayo Mtakatifu 2:1-6 unaosimuliwa habari za kuzaliwa kwa Yesu Kristo katika mji wa Bethlehemu.

Katik utamaduni wa kumsifu Mungu kwa nyimbo, amesema hatua zote za unabiii hadi kuzaliwa kwa kristo zilitawaliwa na ishara za kumsifu Mungu kwa nyimbo.

Amesema Bikra Mariamu alimwimbia Mungu baada ya kupokea salamu za kubeba ujauzito wa kristo huku malaika na wachungaji wakimsifu Mungu kwa nyimbo, sawa na Simeon baada ya kutimiza unabii.

Pili, ni kuenzi maisha ya upendo wa Mungu kwa mwanadamu aliyefanya neno kuwa mwili kwa lengo la kukamilisha fumbo la ukombozi wa dunia kupitia kuzaliwa kwa kristo.

Jambo la tatu la kujifunza kwa Wakristo duniani ni hali ya uvumilivu na kukuza kiwango cha Imani yao kupitia kwa Bikra Mariamu aliyepokea taarifa ngumu za kubeba mimba bila kumjua mwanaume.

Kila ifikapo Disemba 25 kila mwaka, mamilioni ya wakristo duniani husherehekea kumbukumbu hiyo iliyosimuliwa katika vitabu mbalimbali vya Biblia takatifu.

Akifafanua zaidi kuhusu kuzaliwa kwa Yesu, Lwiza amefanya marejeo ya Kitabu cha Mathayo Mtakatifu 2:1-6 kinachosema, Yesu alizaliwa mjini Bethlehemu, mkoani Yudea, wakati Herode alipokuwa mfalme.

“Punde tu baada ya kuzaliwa kwake, wataalamu wa nyota kutoka mashariki walifika Yerusalemu, wakauliza, yuko wapi mtoto aliyezaliwa?”

“Mfalme wa Wayahudi, aliyezaliwa? Tumeiona nyota yake ilipotokea mashariki, tukaja kumwabudu. Mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika.”