Watoto wasombwa na maji ya mto uliofurika ghafla wakiogelea
Muktasari:
Wanafunzi wawili wa darasa la pili katika Shule ya Msingi Terita Wilaya ya Butiama mkoani Mara wamekufa baada ya kusombwa na maji ya Mto Suguti uliofurika ghafla walipokuwa wakiogelea.
Butiama. Wanafunzi wawili wa darasa la pili katika Shule ya Msingi Terita Wilaya ya Butiama mkoani Mara wamekufa baada ya kusombwa na maji ya Mto Suguti uliofurika ghafla walipokuwa wakiogelea.
Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Moses Kaegele amesema ajali hiyo imetokea jana Desemba 3, 2023 wakati watoto hao Buchunnga Luhuye (10) na Joseph Mgema (10), wote wakazi wa Kijiji cha Mwibagi Wilaya ya Butiama walipokuwa akiogelea kama ilivyo kawaida yao wakiwa machungani.
Amesema watoto hao walikwenda kuchunga ng'ombe ndipo wakaamua kuogelea wakati mto ukiwa na maji ya kawaida lakini ghafla maji yalianza kufurika kutokana na mvua kunyesha sehemu za milimani hivyo kuzamishwa pasipo wao kujua.
"Walikuwa wanaogelea kwenye maji ya kawaida bila kufahamu kuwa kuna mvua kubwa iliyonyesha maeneo ya milima ya Mwibagi iliko chanzo cha Mto Suguti; ghafla maji yaliongezeka na kuwazidi nguvu,’’ amesema Kaegele
Amesema mwili wa mtoto mmoja tayari umepatikana huku juhudi zikiendelea kuutafuta mwili wa mtoto mwingine.
Mkuu huyo wa Wilaya amewataka wazazi na walezi kuwa waangalifu kwa kufuatilia nyendo za watoto wao wawapo machungani katika kipindi hiki cha mvua.
"Wazazi na walezi tuwaonye watoto wetu dhidi ya tabia ya kupenda kuogelea mtoni kwa sababu maji huongezeka ghafla nyakati hizi za mvua,’’ amesema Kaegele