Wazazi wenye uchu wa mahari kikaangoni

  • Katibu Tawala wilaya ya Serengeti Cosmas Qamara akizindua wiki ya Mahakama, kulia ni Hakimu mkazi mfawidhi Ismael Ngaile.

Muktasari:

Serikali kuwashughulikia wanafanya vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Serengeti. Wazazi na walezi wanaoendeleza vitendo vya ukatili wa kijinsia vikiwamo vya ukeketaji na kuwaozesha watoto wadogo wataendelea kushughulikiwa kwa mjibu wa sheria.

Katibu Tawala wilayani Serengeti, mkoani Mara Tanzania, Cosmas Qamara ameyasema hayo leo Jumapili Januari 24, 2021 alipokuwa akizindua Wiki ya Sheria wilayani humo.

Amesema vitendo hivyo ni sawa na kwenda kinyume cha Sheria na Haki za Binadamu.

“Kuna ukatili mkubwa unaendelea wa watoto wa kike na wanawake unaotokana na mila zenye madhara, nawaambia acheni maana sisi tukikukamata tutakufikisha mahakamani na kuadhibiwa kwa mujibu wa sheria zilizowekwa, hivyo nawaambia badilikeni,” amesema Qamara.

Amewataka wananchi kuheshimu uamuzi utolewao na Mahakama ambayo hutenguliwa na ngazi ya juu ya muhimili huo na si ofisi ya mkuu wa wilaya.

  • Maandamano yaliyoshirikisha wanafunzi na wadau mbalimbali wa sheria

“Ukishindwa kesi kata rufaa kwa wakati, maana ofisi yetu haiwezi kutengua uamuzi wa mahakama,” amesema.

Pia, Mkuu huyo wa wilaya amewataka wananchi wote wilayani humo kuitumia  wiki hiyo kupata ufafanuzi mbalimbali wa kisheria kwenye mabanda ya maonyesho badala ya kulalamikia pembeni na kwenye vyombo visivyoweza kutengua uamuzi wa kisheria.

Mapema, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya, Ismael Ngaile alisema kwa kushirikiana na wadau mbalimbali watatoa huduma ya msaada wa kisheria na ufafanuzi wa masuala yanayowasumbua wananchi kwa wiki nzima kabla ya siku ya kilele.