Hatimaye Polisi yawalinda Bawacha

Muktasari:

  • Wakati Baraza la wanawake Chadema (Bawacha) likijiandaa kuanza maandamano, Jeshi la Polisi limeimarasha ulinzi.

Dar es Salaam. Wakati Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) wakiwa wamekusanyika kwenye viwanja vya posta ya zamani ili kuanza maandamano yao, Jeshi la Polisi limeimarasha ulinzi kuzunguka viwanja hivyo.

Mei 7 mwaka huu Baraza hilo likitangaza kufanya maandamano ya kushinikiza Spika wa Bunge Dk Tulia Ackson kuwaondoa wabunge 19 ambao wameshafukuzwa uanachama na kupoteza sifa ya kuwa wabunge.

Hata hivyo siku mbili baadae walitangaza kusogeza mbele maandamano hayo hadi Mei 11, kutokana na barua waliyoipeleka  polisi kuomba ulinzi, kukosewa.

Taarifa iliyotokewa jana na Katibu Mkuu wa Bawacha Catherine Ruge ilieleza kuwa Jeshi la Polisi limewaruhusu kwa kuwa maandamano hayo ni ya amani, hivyo watakuwepo kuhakikisha kuna amani, utulivu na usalama.

Maandamano hayo kwa mujibu wa uongozi wa Bawacha, yataanzia Posta ya zamani na kuhitimishwa katika ofisi ndogo za Bunge zilizopo mtaa wa Shaban Robert jijini Dar es Salaam.

Hata alipotafutwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Muliro Jumanne kutolea ufafanuzi taarifa hiyo alijibu kwa kifupi tutaona hiyo kesho.

Mwanachi Digital imefika kwenye viwanja hivyo na kushuhudia Bawacha wakiwa wamekusanyika, wakiwa na mabango yenye jumbe mbalimbali.

Licha ya ulinzi kuimarishwa kuzunguka viwanja hivyo pia Askari wameimarisha ulinzi kwenye barabara ya Sokoine ikiwa imefungwa na Askari wote wakiwa wakike.

Maandamano hayo  ya Bawacha yanafanyika licha ya , Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuwaandikia barua ikiwashauri kusitisha kwa kuwa jambo wanalolilalamikia liko mahakamani.

Juzi Msajili Msaidizi wa Vyama vya Siasa nchini, Sisty Nyahoza alikiri kuwaandikia barua bawacha, akiwashairi kusitisha maandamano hayo kwa kuwa kesi bado ipo mahakamani.

Hili linafanyika ikiwa kesi ya wabunge hao kupinga kuvuliwa uanachama ikiendelea katika Mahakama Kuu, Masjala kuu ya Dar es Salaam na inatarajiwa kutajwa tena Mei 17, mwaka huu.