Kiungo mwili jumba katua Simba

Kiungo mwili jumba katua Simba

Muktasari:

  • SIMBA wanasajili tu na hawaachi kitu baada ya hivi karibuni kunasa saini ya kiungo fundi wa Kagera Sugar, Mzanzibar Abdul Samad waliyempa mkataba wa maika miwili.

SIMBA wanasajili tu na hawaachi kitu baada ya hivi karibuni kunasa saini ya kiungo fundi wa Kagera Sugar, Mzanzibar Abdul Samad waliyempa mkataba wa maika miwili.

Katika ripoti ya kocha wa Simba, Didier Gomes alipendekeza kuhitaji kiungo mchezeshaji lakini mwenye uwezo wa kukaba na kushambulia kwa pamoja kama alivyo Aliou Dieng anayecheza Al Ahly ya Misri.

Mwanaspoti limejiridhisha kuwa uongozi wa Simba, umelifanyia kazi pendekezo hilo na wametua kwa Samad ambaye amesaini mkataba wenye thamani ya Sh35 milioni.

Samad mwenye uwezo wa kumiliki mpira pamoja na kukaba kwa nguvu, inaelezwa tayari ameshamwaga wino wa kuwatumikia mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara na wakati wowote atajiunga na timu hiyo tayari kujiandaa na msimu mpya wa ligi na mashindano ya kimataifa.

Inaelezwa Simba wamemalizana kimya kimya na Samad kutokana na mapendekezo ya Gomes anayetaka kiungo mwenye sifa kama zake ili aje kucheza pamoja na Taddeo Lwanga.

Msimu huu, miongoni mwa viungo waliokuwa kwenye viwango bora, Samad ni mmoja wao akiwa na sifa kubwa ya kukaba na matumizi ya nguvu lakini pia ni bora pia anapokuwa na mpira wakati timu ikishambulia.

Mwanaspoti lilimtafuta Samad aliyeko mapumzikoni nyumbani kwao Zanzibar ambaye alikiri kumalizana na Simba na tayari ameshamwaga wino kuichezea timu hiyo msimu ujao.

“Nimemalizana nao, sasa najipanga kuja Dar es Salaam tu kujiunga na timu kwaajili ya msimu ujao,” alisema Samad ambaye alianza soka la ushindani katika timu ya Jang’ombe Boys kisha kwenda Stand United, Malindi na Kagera Sugar.

Wakati huo huo, inaelezwa Gomes amependekeza pia kusajiliwa kwa kiungo mmoja raia wa Mali lakini viongozi wa Simba wamemgomea baada ya kutoridhika na kiwango chake.