Kongamano la Kakama, maadhimisho ya Kiswahili Burundi kutoa mwelekeo mpya
Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili Afrika Mashariki (Kakama), Dk Caroline Asiimwe akizungumza na waandishi wa habari nchini Burundi leo Julai 4, 2026.
Muktasari:
- Kongamano la Tatu la Kakama linatarajiwa kufanyika kesho Julai 5 na 6 nchini Burundi, litafuatiwa na Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani Julai 7.
Burundi. Wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wametakiwa kushiriki kikamilifu ili kuweza kufikia malengo ya mwelekeo mpya ulioanzishwa na Kamisheni ya Kiswahili ya jumuiya ya Afrika Mashariki (Kakama) katika kuhakikisha akili unde inatumika kuleta maendeleo ya Kiswahili.
Kakama imeazimia kuanzisha mwelekeo huo mpya ili kufikia mafanikio kupitia Komangano la Kimataifa la Tatu ambalo linaanza kesho Jumapili Julai 5, 2026 na maadhimisho ya Siku Kiswahili Duniani Julai 7, ambapo kwa pamoja yanafanyika Bujumbura nchini Burundi.
Akizungumza na waandishi wa habari, jijini Bujumbura leo Jumamosi Julai 4, 2026, Katibu Mtendaji wa Kakama, Dk Caroline Asiimwe amesema kila nchi wanachama zinatakiwa kushiriki kikamilifu ili kufikisha azma ya Kakama kuleta maendeleo ya Kiswahili katika teknolojia ya akili unde pamoja wingi lugha kama inavyosema kaulimbiu ya mwaka huu.
Amesema maeneo yanayotakiwa kutiliwa mkazo ni kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano.
Ametoa wito uwekezaji zaidi ufanyike kwenye maeneo mbalimbali ikiwamo kampuni za kuzalisha maudhui ya Kiswahili kwa kutumia akili unde, kubuni mifumo mbalimbali na kuongeza ushirikiano wa kibunifu wa kikanda.
"Ninatoa wito kwa wana Afrika Mashariki kushiriki kwa namna mbalimbali ikiwemo kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano," amesisitiza Dk Asiimwe.
Amesema watunga sera pia wanalojukumu kutumia fursa hiyo kwenye nchi wanachama kuhimiza sera zinazochochea matumizi ya teknolojia ya akili unde.
Dk Asiimwe amewakaribisha wana Afrika Mashariki kutoka kada mbalimbali kushiriki kongamano hilo kwa namna mbalimbali ikiwemo kufika kwenye mkutano na kufuatilia mitandaoni.
Amesema kongamano hilo linakwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 10 ya Kamisheni ya Kiswahili tangu kuazishwa kwake.
Amewataka wanajuiya ya Afrika Mashariki kujivuvia mafanikio mbalimbali yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa kamisheni hiyo.