VIDEO: Mbowe, Matiko wapata dhamana, warejea uraiani
Muktasari:
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam leo Alhamisi imemwaachia kwa dhamana Kiongozi wa Upinzani nchini Tanzania, Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime Mjini (Chadema), Esther Matiko
Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe na mhazini wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Esther Matiko wamerejea uraiani baada ya kushinda rufaa yao Mahakama Kuu Dar es Salaam.
Hukumu hiyo imetolewa leo mchana Alhamisi Machi 7, 2019 na Jaji Sam Rumanyika,
Wakati Jaji Rumanyika akisoma hukumu hiyo ulinzi mahakamani hapo ulikuwa umeimarishwa kwa askari wengi waliotanda sehemu mbalimbali za Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Mbowe na Matiko walikata rufaa Mahakama Kuu wakipinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwafutia dhamana, kwa sababu za kushindwa kufika mahakamani hapo bila sababu za msingi kwa ajili ya kesi yao ya jinai inayowakabili mahakamani hapo wao na viongozi wengine saba wa chama hicho.
Walifutiwa dhamana hiyo na aliyekuwa Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri Novemba 23, 2018 lakini siku hiyohiyo kupitia kwa wakili wao Peter Kibatala walikata rufaa Mahakama Kuu chini ya hati ya dharura sana wakipinga uamuzi huo.
Endelea kufuatilia Mwananchi kujua undana wa habari hii