Msiba wa Tanzania ulivyoteka vyombo vya habari vya nje

Muktasari:

Ajali hiyo ilitokea katika eneo la karibu na kituo cha mabasi cha Msamvu baada ya lori la mafuta kupinduka na kuwaka moto muda mfupi baada ya watu kuanza kuchota mafuta.

Dar es Salaam. Ajali ya moto ilitotokea nchini Tanzania na kusababisha watu 69 kufariki dunia na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa imeteka vyombo mbalimbali duniani.

Ajali hiyo ilitokea jana Jumamosi Agosti 10, 2019 katika mtaa wa Itigi, Msamvu mkoani Morogoro mita 200 kabla ya kufika kituo cha mabasi cha Msamvu barabara ya Morogoro- Dar es Salaam baada ya lori la mafuta kupinduka na kuwaka moto muda mfupi baada ya watu kuanza kuchota mafuta.

Kufuatia ajali hiyo vyombo mbalimbali vya kimataifa viliripoti msiba huo huku Shirika la habari la BBC ambalo kwa siku ya jana liliripoti moja kwa moja kinachoendelea katika tukio hilo.

BBC kwa siku nzima ya jana ilikuwa ikirusha matangazo yake moja kwa moja na kuwahabarisha wasomaji wake kila kilichokuwa kikiendelea katika eneo la tukio katika juhudi za kuokoa maisha ya watu waliopatwa na mkasa huo.

Wengine ni Idhaaa ya Kiswahili ya DW, Shirika la utangazaji la Al Jazeera, magazeti ya Afrika Mashariki ikiwamo Daily Nation na Taifa Leo ya Kenya pamoja na Daily Monitor la nchini Uganda.

Mbali na vyombo hivyo vya habari kuripoti tukio hilo, raia wa mataifa mbalimbali waliungana na Watanzania kuwapa pole na kuwafariji kupitia mitandao ya kijamii.

Kupitia ukurasa wa twitter Shawn Rickey alisema “ni tukio la uchungu kwa Watazania, nawapa pole sana.”

Mwingie Darrell Howard alitaka Serikali ya Tanzania kuchukua hatua kwa wote waliosababisha uzembe huo. Wakati Dwayne Marvin aliwapa pole wafiwa wote na kuwaombe majeruhi wapate nafuu haraka.

Mapema jana Rais wa Tanzania, John Magufuli aliwatembelea  majeruhi 43 wa ajali hiyo waliolazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na kuwapatia kila mmoja Sh500,000 kwa ajili ya matumizi mbalimbali.

Majeruhi 46 waliokuwa wamelazwa katika hospitali ya Mkoa wa Morogoro walihamishiwa katika hospitali hiyo. Hata hivyo, watatu kati yao wamefariki dunia leo.

Akiwa katika wodi ya Sewahaji na Mwaisela, alizungumza na majeruhi hao kuwashukuru wauguzi pamoja na madaktari kwa huduma nzuri na kuwazawadia Sh1 milioni.