VIDEO: Profesa Kabudi azungumzia Zimbabwe kuondolewa vikwazo vya kiuchumi
Muktasari:
Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi amekabidhiwa rasmi uenyekiti wa baraza la mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kugusia nchi ya Zimbabwe kuondolewa vikwazo vya kiuchumi.
Dar es Salaam. Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi amekabidhiwa rasmi uenyekiti wa baraza la mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kugusia nchi ya Zimbabwe kuondolewa vikwazo vya kiuchumi.
Makabidhiano hayo yamefanyika leo Agosti 13, 2019 mbele ya Sekretarieti ya SADC, na Profesa Kabudi kuchukua nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na naibu waziri mkuu na waziri wa mambo ya nje wa Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah.
"Katika kipindi chetu tutahakikisha jumuiya ya kimataifa kuondoa vikwazo vya kiuchumi Zimbabwe. Lazima viondolewe kwa kuwa kiongozi aliyekuwepo ameshaondoka madarakani na wananchi wanaendelea vizuri kwa sasa,” amesema Profesa Kabudi.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa, Profesa Kabudi amesema Tanzania katika kipindi hicho cha mwaka mmoja wa uongozi wake, itatekeleza kauli mbiu ya maendeleo shirikishi ya viwanda, kuongeza ajira pamoja na kusimamia kwa weledi masuala ya watoto, wanawake na afya.
"Tutazingatia suala la maendeleo endelevu na kuhakikisha tunaongeza viwanda, ajira pia asilimia 60 ya raia katika nchi 16 za SADC ni vijana hivyo lazima kuhakikisha tunaendeleza ajira," amesema.
Profesa Kabudi amesema suala muhimu kwa sasa ni kuhakikisha Kiswahili kinakuwa lugha rasmi ya SADC kwa kukuza lugha hiyo ambayo kwa sasa ni ya Tisa duniani.