Profesa Lipumba amshangaa Lowassa kutimka Mbowe akiwa gerezani

Muktasari:

Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema hajastushwa na uamuzi wa Edward Lowassa kurejea CCM lakini ameshangaa uamuzi huo kuuchukua wakati mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akiwa gerezani

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema anashangazwa na uamuzi wa Edward Lowassa kurejea CCM katika kipindi ambacho mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akiwa gerezani.

Akizungumza na Mwananchi jana Ijumaa Machi 1, 2019, Profesa Lipumba, ambaye mwaka 2015 alijivua uenyekiti kutokana na CUF kuunga mkono Lowassa kugombea urais kwa mgongo wa vyama vinne, amesema hajashangazwa na hatua ya Lowassa kurejea CCM kwa kuwa alijua ingawa hakufahamu siku.

"Lowassa amerudi CCM bila aibu. (Amerudi) wakati Mbowe bado yupo gerezani. Hakufikiria wenzake anawaachaje," alisema Profesa Lipumba.

Mbowe pamoja na mbunge wa Tarime, Esther Matiko, yupo Segerea tangu Novemba 23, 2018 baada ya dhamana yao katika kesi ya jinai inayowakabili pamoja na viongozi wengine wa Chadema, kufutwa.

Katika mazungumzo yake na Mwananchi, Profesa Lipumba alisema kila wakati aliwaeleza Watanzania kuwa Lowassa ni mgombea wa nafasi ya urais wa CCM na si John Magufuli kama watu walivyodhani.

"Leo imedhihirika sasa hata alipokuja yule mganga wa Nigeria (kiongozi wa kanisa la Church for All Nation la Nigeria, TB Joshua) kukutana nao kwa nyakati tofauti niliwahi kusema suala hili. Leo Watanzania watakuwa mashahidi kwa Lowassa kurejea,” alisema

Alisema ni vyema wapinzani wakawa na msimamo na kwamba mapambano ya kudai haki yanahitaji muda mrefu si harakaharaka kama walivyofanya Chadema kumchukua Lowassa ili awasaidie kuchukua nchi.

"Niliwaambia Lowassa amekuja upinzani kwa ajili ya madaraka tu. Hiki cha leo ni dhambi ya usaliti waliomfanyia (katibu wa zamani wa Chadema, Willbrod) Dk Slaa inaanza kuwatafuna,” alisema

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, Lowassa aligombea urais kupitia Chadema na kuungwa mkono na vyama vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi vya NLD, NCCR-Mageuzi na CUF.