Wananchi watakiwa fuatilia utabiri wa hali ya hewa
Muktasari:
Hatua hiyo imeelezwa itasaidia kujiandaa kwa kilimo na kuchukua tahadhari pindi mvua zinapoanza kunyesha
Dar es Salaam. Katibu Mkuu ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Uratibu, Profesa Faustin Kamuzora amesisitiza kufuatiliwa kwa taarifa za hali ya hewa ili kujiandaa kukabiliana na majanga yanayoweza kujitokeza.
Profesa Kamuzora ameyasema hayo leo Septemba 18,2018 wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya programu ya kidunia ya huduma za hali ya hewa.
Amesema sayansi iliyopo sasa inaweza kutoa utabiri wa hali ya hewa ambao kwa kiasi kikubwa matokeo yake yana ukweli.
"Hawa wenzetu wa mamlaka ya hali ya hewa sasa wanatoa taarifa ambazo kiwango cha ukweli wake kimekuwa kikiongezeka kila siku.
"Tuwe tunafuatilia taarifa hizi ili tujue tunaishi vipi hasa kwa wakulima ni muhimu kuangalia upande nini kwa wakati gani na ujiandae vipi kulingana na hali ya hewa," amesema
Profesa Kamuzora amesema: "Ukiwa umejiandaa na maafa yakitokea athari zake haziwezi kuwa kubwa sana, kuna vitu unaweza kuokoa."