Halima Mdee atinga bungeni, Spika Ndugai atoa onyo

Mbunge wa Kawe Halima Mdee (Chadema) akiuliza swali bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

  • Aprili 2, 2019, Mbunge wa Upinzani nchini Tanzania kupitia Chadema, Halima Mdee, alisimamishwa kuhudhuria mikutano miwili ya Bunge hilo kwa tuhuma za utovu wa nidhamu.
  • -Adhabu hiyo ilianza Aprili 2, 2019 wakati wa mkutano wa 15 wa Bunge la Bajeti pamoja na mkutano wa 16 uliofanyika Septemba.

Dodoma. Mbunge wa Kawe (Chadema) nchini Tanzania, Halima Mdee amesimamisha shughuli za Bunge kwa dakika moja baada ya kuingia bungeni huku Spika wa Bunge hilo, Job Ndugai akiwaonya wabunge wa upinzani kuwa watamponza.

Mdee ameingia bungeni leo Jumatatu Novemba 11,2019 saa 3:44 asubuhi wakati Bunge likiendelea na shughuli lakini wabunge wa upinzani walianza kugonga meza huku yeye akipita katika maeneo yao na kuwapa mikono.

Kitendo hicho kilifanya Naibu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe kusimama kwa muda ili kupisha kelele za makofi ya upinzani wakati yeye (Halima) akiwa amefika mezani kwa Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi), James Mbatia na kusalimiana kwa kukumbatiana.

Mdee alikuwa nje ya Bunge baada ya Spika  Ndugai kumsimamisha kutokana na kauli yake ya kuunga mkono kauli ya aliyekuwa Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali Profesa Mussa Asad aliyosema bunge ni dhaifu.

Kosa hilo pia lilimuangukia mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbles Lema ambaye atakuwa nje ya bunge hadi mkutano wa 18 wa bungeni mapema mwakani.

Spika Ndugai aliwaambia wabunge kuwa makofi ya wapinzani yanaweza kumponza tena Mdee.

"Naomba mtulie, hizo kelele zinaweza kumponza mwenzenu ohoo si mnanijua, not jocking (siyo utani) haya shauri yenu," amesema Ndugai.

Kauli ya Ndugai ikimfanya Mdee kusimama na kuinama mbele ya kiti cha Spika kuashiria heshima kwa kiti na kisha akaa kitini kwake ndipo Naibu Waziri Bashe akaendelea na majibu ya swali lililoulizwa kwake.