Mawigi na rasta kuanza kutozwa kodi

Muktasari:

Serikali imewaongezea gharama wanaopenda kuvipamba vichwa vyao kwa nywele za bandia hasa mawigi na rasta za bei mbaya

Dar es Salaam. Serikali imependekeza kutoza ushuru wa asilimia 10 kwenye nywele za bandia zinazotengenezwa nchini na asilimia 25 kwa zinazoagizwa kutoka nje.

Ushuru huo, utaanza kutozwa Julai Mosi hivyo wapenzi wa nywele hizo wanatakiwa kujipanga kulipa zaidi ili kuendelea kuwa nazo hasa mpya zitakazoingizwa au kutengenezwa kuanzia saa.

Ushuru huo, Serikali imesema “unakusudia kuongeza mapato.”

Wakati ikiwaongezea gharama wapenda nywele hizo na mawigi maarufu kama yatokayo Brazil au Peru, Serikali imesamehe ushuru wa vilainishi vya ndege vinavyoingizwa nchini na mashirika yanayotambulika katika mikataba ya kimataifa ya huduma za usafiri wa anga.

“Lengo la hatua hii ni kuiwezesha nchi yetu kusaini mikataba ya kimataifa ya huduma za anga ambayo ilishindikana kusainiwa hapo awali,” amesema Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango.

Dk Mpango amesema hayo leo Juni 13, 2019 alipokuwa anawasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2019/20.

Vilevile, Serikali imependekeza kutoza ushuru wa asilimia 10 kwenye mabomba na vifaa vya plastiki vinavyotumika kwenye miradi ya ujenzi wa miundombinu ya maji kwa kuwa hivi sasa kuna viwanda vingi vyenye uwezo wa kuzalisha bidhaa hizo kutosheleza mahitaji nchini.