Mbatia apigwa ‘stop’ kuendelea na kampeni kwa siku saba

Mgombea ubunge wa Vunjo mkoani Kilimanjaro, James Mbatia

Muktasari:

Mgombea ubunge wa Vunjo mkoani Kilimanjaro, James Mbatia amesimamishwa kufanya kampeni kwa siku saba baada ya kukutwa na hatia ya kutumia kipeperushi ambacho hakijaidhinishwa na msimamizi wa uchaguzi.

Moshi. Kamati za maadili zimeendelea kuwa mwiba kwa wagombea na safari hii mgombea ubunge wa Vunjo kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi, James Mbatia amesimamishwa kufanya kampeni kwa siku saba, kuanzia leo Oktoba 17 hadi 23, 2020.

Mbatia ambaye pia ni mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi amethibitisha kusimamishwa kuendelea na kampeni leo Oktoba 17,2020 baada ya  kukabidhiwa barua.

“Ni kweli wamenisimamisha lakini nimeshangaa maana walipotaka nipeleke utetezi kuhusu hicho kipeperushi tuliwapelekea na ushahidi wa barua iliyokitambulisha hicho kipeperushi,” amesema Mbatia.

Barua ya mwenyekiti wa kamati ya maadili jimbo la Vunjo, Michael Mwandezi inaeleza kuwa Mbatia amesimamishwa kufanya kampeni kutokana na kutumia kipeperushi ambacho hakijaidhinishwa na msimamizi wa uchaguzi.

Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, kamati ya maadili katika kikao chake cha Oktoba 16, 2020 ilikaa na kupitia tuhuma za uvunjifu wa maadili ya uchaguzi na kumkuta na hatia ya kukiuka maadili hayo.