Mfungwa agoma kutoka gereza la Ruanda, ajijeruhi

Muktasari:

Merad Abraham, mfungwa katika gereza la Ruanda mjini Mbeya aliyeachiwa huru kwa msamaha wa Rais John Magufuli amegoma kutoka gerezani kwa maelezo kuwa hana pa kwenda.

Mbeya. Merad Abraham, mfungwa katika gereza la Ruanda mjini Mbeya aliyeachiwa huru kwa msamaha wa Rais John Magufuli amegoma kutoka gerezani kwa maelezo kuwa hana pa kwenda.

Mbali na kukataa kutoka gerezani, Abraham alichukua uamuzi wa kujijeruhi katika paji  la uso kwa jiwe licha ya kutakiwa kutofanya hivyo na askari.

Abraham ni kati ya wafungwa 5,533 waliopata msamaha wa Rais Magufuli  jana Jumatatu Desemba 9, 2019 katika maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa Tanganyika yaliyofanyika katika uwanja wa CCM Kirumba mkoani Mwanza.

Abraham ambaye alihukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la kubaka, alikuwa ametumikia miaka 19 jela.

Mfungwa huyo alijijeruhi baada ya mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila kuondoka  katika gereza hilo baada ya kushuhudia  wafungwa 70 kati ya 259 wa gereza hilo wakikamilisha taratibu za kutoka.

Abraham alirejeshwa katika gereza hilo licha ya kujijeruhi na kusubiri utaratibu wa kutoka kesho pamoja na wenzake.