Mgambo anayedaiwa kuwapa adhabu wanafunzi na kusababisha vifo asakwa

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Sweetbert Njewike

Muktasari:

  • Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida linamsaka mkufunzi msaidizi wa Jeshi la Akiba la Mgambo, Said  Ng’imba kwa madai ya kutoa adhabu kwa wanafunzi wawili na kusababisha vifo vyao.

Singida. Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida linamsaka mkufunzi msaidizi wa Jeshi la Akiba la Mgambo, Said  Ng’imba kwa madai ya kutoa adhabu kwa wanafunzi wawili na kusababisha vifo vyao.

Waliofariki dunia ni Emmanuel Hamisi (20) mkazi wa kijiji cha Mudida na Ismael Hussein (22) mkazi wa kijiji cha Sepuka waliokuwa wanahudhuria mafunzo ya awali ya Mgambo yanayoendelea katika  kijiji cha Mudida.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa Novemba 22, 2019 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Sweetbert Njewike amesema tukio  hilo limetokea Novemba 20, 2019.

Amesema wanafunzi hao walipewa adhabu ya kuingia katika dimbwi la maji kutokana na kutohudhuria mafunzo ya Novemba 19.

“Polisi likishirikiana na Jeshi la Uokoaji na Zimamoto walishirikiana kuwaokoa lakini walikuwa wameshafariki dunia.”

“Ilipobainika kuwa walipozama hawakuonekana mkufunzi huyo alikimbia. Tumeanza kumtafuta naamini tutamkamata tu,” amesema kamanda huyo.