Mwanamke adaiwa kujinyonga hadi kufa baada ya kumuua mwanaye

Waombolezaji wakiwa nyumbani kwa Maneno Kapunda kufuatia kifo cha Efrazia Maneno (22)na mwanae Regina Steven mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili

Muktasari:

Efrazia Maneno (22), mkazi wa kijiji cha Nyaseke kata ya Bulela mjini Geita nchini Tanzania anadaiwa kumuua kwa kumnyonga mwanae mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili kisha naye kujinyonga.


Geita. Efrazia Maneno (22), mkazi wa kijiji cha Nyaseke kata ya Bulela mjini Geita nchini Tanzania anadaiwa kumuua kwa kumnyonga mwanae mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili kisha naye kujinyonga.

Tukio hilo limetokea jana Jumapili Agosti 18, 2019 saa saba mchana umbali wa mita 300 kutoka nyumba aliyokuwa akiishi, alitumia khanga kujinyonga katika mti wa mwembe.

Maneno Kapunda,  baba mzazi wa Efrazia amedai binti yake alikua akiishi na babu na bibi baada ya wazazi kutengana na hakueleza tatizo lolote kabla ya kufanya uamuzi wa kujiua

“Huyu binti yangu alimaliza shule ya Sekondari Bulela akiwa mjamzito na mwanaume aliyempa mimba alikataa hivyo alibaki hapa nyumbani na wazee kwa kweli tukio hili limenishangaza,” amesema Kapunda

Ofisa mtendaji wa kijiji cha Nyaseke, John Maguta amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema polisi walifika jana jioni Jumapili na kutoa mwili uliokuwa ukining’inia na kuruhusu familia kuendelea na taratibu za mazishi yanayotarajiwa kufanyika leo Jumatatu kijijini hapo.

Jitihada za kumpata kamanda wa polisi mkoa wa Geita zinaendelea ili aweze kuzungumzia tukio hilo.

Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Geita Dismas Kisusi ameieleza Mwananchi kwa njia ya simu kuwa ni kweli tukio hilo limetokea na kwamba mwanamke huyo alimnyonga mwanae kwa kitambaa kisha naye kujinyonga

“Hakuna uchunguzi unaofanyika maana mhusika mkuu amekufa na hata tukichunguza sio rahisi kupata ufumbuzi, “amesema Kisusi

Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi