Profesa Jay apagawisha 'birthday' Lady Jay Dee

Muktasari:

Mbunge wa jimbo la Mikumi na mwanamuziki mkongwe wa muziki wa kizazi kipya Joseph Haule maarufu Profesa Jay, ameuteka usiku wa mkongwe Judith Wambura ‘Ladyjaydee’ baada ya kuwafanya mashabiki walipuke kwa shangwe kufuatia vibao vyake vya zamani.

Dodoma. Unaweza kusema ni kama ndoto, lakini ndivyo ilivyokuwa pale Profesa J na Lady Jay Dee walipovamia jukwaa pamoja hali iliyowafanya mashabiki kulipuka kwa shangwe na  kuvamia 'dancing floor' kusindikiza show ya wawili hao.

Profesa J ambaye alikuja kunogesha sherehe ya miaka 20 ya Lady Jay Dee tangu aanze muziki, alipanda jukwaani leo Jumapili saa 6:52 akimsindikiza Lady Jay Dee.

Lady Jay Dee alipanda jukwaani Jumamosi ya saa 5:24 akiwa kwenye vazi lililounganika suruali na blauzi lililoshonwa kwa kuunganisha na joho.

Vazi hilo lenye rangi nyeusi joho lake lilikuwa na mkia mrefu uliokuwa umebebwa na wapambe usiguse sakafu kama vile joho la malkia linavyobebwa.

Msanii huyo ambaye ni legendary aliingia jukwaani taratibu akiimba wimbo wake wa machozi ambao uliibua hisia za mashabiki wake waliojimwaga jukwaani kumsindikiza.

"Mmenisema sana jamani... Nimechoka," ndivyo Lady J Dee alivyokonga nyoyo za mashabiki wake huku akiuliza nani hajawahi kupenda.

"Nimekuwa teja. Teja la mapenzi. Na aliongeza "hata Faiza amewahi kuoenda".

Kitendo cha kumtaja Faiza aliyeingia ukumbini saa 5:28 usiku wa jana Jumamosi aliinuka kwenda kumtunza Lady J  Dee.

Faiza aliingia ukumbini akiwa ameongozana na kijana, alisimama kwa muda ndani ya ukumbi baada ya kukosa sehemu ya kukaa kutokana na watu kujaa ukumbini hadi wengine kukaa chini.

Hata hivyo, Faiza alipewa kiti yeye na aliyeongozana naye.

Faiza alikuwa amevalia kaptura yenye rangi ya kijani iliyopauka na blauzi lenye rangi ya cream. Na iliyompendeza kulingana na mwili wake.