J.Lo, mumewe kulipamba jumba lao la Sh150 bilioni

Muktasari:

Wanandoa hao wa Hollywood walitumia miaka miwili kutafuta kiota hicho kipya kwa ajili ya penzi lao, kwa mujibu wa Wall Street Jounal, jumba hilo lina vyumba 12 vya kulala, bafu 24, majiko 15, sehemu ya kuegesha magari 12, viwanja vya michezo n.k.

Mwimbaji Jennifer Lopez (J.Lo) na mume we, Ben Affleck wameonekana wakifanya manunuzi ya samani kwa ajili ya jumba lao jipya la kifahari lenye thamani ya Dola 60 milioni, wastani wa Sh150 bilioni.

Jumba hilo la kifahari lina vyumba 12 vya kulala, bafu 24, majiko 15, sehemu za kuegesha magari 12, viwanja vya michezo n.k.

Lopez, 54, na Affleck, 51, walipigwa picha huko Los Angeles, Marekani Jumamosi iliyopita wakiwa ndani ya duka kubwa wakati wakichagua bidhaa zao kabla ya kuketi na kufanya mazungumzo mafupi. 

Walitazamana machoni kwa furaha huku wakizungumza kisha walikumbatiana walipokuwa wakijaribu kochi katika duka hilo, ni kama walijaribu kupata furaha kabla ya kufanya manunuzi hayo ambayo kiasi chake bado hakijatajwa.

Hatua hiyo inakuja takribani miezi sita baada ya wawili hao kutoa fedha taslimu kiasi cha Dola 60.85 milioni kwa ajili kununua jumba hilo lililopo mitaa ya Beverly Hills, California.

Wanandoa hao wa Hollywood walitumia miaka miwili kutafuta kiota hicho kipya kwa ajili ya penzi lao, kwa mujibu wa Wall Street Jounal, jumba hilo lina vyumba 12 vya kulala, bafu 24, majiko 15, sehemu ya kuegesha magari 12, viwanja vya michezo n.k.

Lopez na Affleck walikuwa na uhusiano mwaka 2002 hadi 2004 walipoachana, Lopez akaenda kufunga ndoa na Marc Anthony (2004 - 2014) na kujaliwa watoto wawili, huku Affleck akimuoa Jennifer Garner (2005 - 2018) na walijaliwa watoto watatu.

Walikuja kurudiana Julai 2021 ikiwa ni 17 ya utengano, walichumbiana kwa mara ya pili Aprili 8, 2022 na walifunga ndoa huko Las Vegas hapo Julai 16, 2022 ikiwa ni ndoa ya nne kwa Lopez.

"Sisi ni wazee kwa sasa, tuna akili zaidi, tuna uzoefu zaidi, tupo eneo tofauti katika maisha yetu, tuna watoto sasa na tunapaswa kuwa makini na mambo hayo," Lopez aliliambia jarida la People mnamo Februari 2022. 

Na katika mahojiano yake mengine na Vogue hapo Novemba 2022, Lopez alisema amebadilisha jina lake la mwisho baada ya kuolewa na Affleck, alieleza kuwa watu bado watamuita 'Jennifer Lopez' ila jina lake halali kwa sasa ni 'Mrs. Affleck'. Kuwa mume na mke kwa kipindi hiki ni kitu anachojivunia.