Maajabu, ziara ya IShowSpeed Afrika
Muktasari:
- Kupitia safari zake katika baadhi ya nchi za Afrika, IShowSpeed amefanikiwa kuvuta hizia za mamilioni ya watu duniani wanaofuatilia live streams zake Afrika
Dar es Salaam. Ziara ya Africa inayofanywa na staa wa mitandao ya kijamii duniani kutokea Marekani, Darren Watkins Jr maarufu IShowSpeed, imeendelea kuacha alama kubwa katika sekta ya burudani, utalii na mitazamo dhidi ya Waafrika.
Kupitia safari zake katika baadhi ya nchi za Afrika, IShowSpeed amefanikiwa kuvuta hizia za mamilioni ya watu duniani wanaofuatilia live streams zake Afrika.
Maajabu yaliyojitokeza kwenye ziara yake ni kuwa baadhi watu Ulaya, walikuwa wanadhani Afrika ni bara linalokabiliwa na umaskini, migogoro na watu wasio staarabika. Lakini ziara hiyo imebadili mitazamo hiyo hasi kwa kiwango kikubwa.
Kupitia video zake, ameonesha Afrika kuwa na vijana wachangamfu, tamaduni, muziki wa kuvutia, chakula cha asili na mazingira mazuri. Hili limechangia kuongeza hamasa ya utalii na kuwafanya vijana wengi wa kimataifa kutamani kutembelea Afrika.
Hili linathibitika katika baadhi ya video na komenti zinazotolewa na watu kutoka mataifa ya nje ya Afrika wakieleza mitazamo yao ya awali ilivyokuwa hasi kuhusu Afrika, huku wengine wakidai hawakuwahi kufahamu kuwa Afrika kuna barabara, maji safi, umeme, majengo makubwa na hata watu wastaarabu.
IShowSpeed ni nani?
Ni mmoja wa watu maarufu zaidi kwenye mitandao ya kijamii duniani, hususan kupitia YouTube ambako ana wafuasi 48.2 milioni, Instagram 43.7 milioni na Tiktok ni 46.1 milioni.
Alizaliwa Januari 21, 2005 nchini Marekani, alianza kujulikana kwa kasi kutokana na video zake za live akicheza games, burudani, muziki na vichekesho. IShowSpeed pia ni msanii wa muziki, akiwa na nyimbo kadhaa zilizopata umaarufu mtandaoni. Hadi sasa tayari ametembelea Angola, South Africa (Afrika Kusini), Mozambique , Eswatini, Botswana, Zimbabwe, Zambia, Rwanda na Kenya