40 wakamatwa wakihusishwa na mauaji ya watu 6 Kilindi
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi ambae pia ni Mkuu wa Operesheni Maalumu za Jeshi la Polisi, Mihayo Msikela
Muktasari:
- Jeshi la Polisi nchini limekamata silaha 11 pamoja na kuwashikilia watu 40 ikiwa ni muendelezo wa kufuatilia waliohusika na mauaji ya watu sita, katika mapigano ya wakulima na wafugaji yaliotokea Kilindi mkoani Tanga Januari 30.
Kilindi. Jeshi la Polisi nchini limekamata silaha 11 pamoja na kuwashikilia watu 40 ikiwa ni muendelezo wa kufuatilia waliohusika na mauaji ya watu sita, katika mapigano ya wakulima na wafugaji yaliotokea Kilindi mkoani Tanga, Januari 30.
Akizungumza na waandishi wa habari katika kituo cha Polisi wilayani Kilindi leo Februari 3, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi ambae pia ni Mkuu wa Operesheni Maalumu za Jeshi la Polisi, Mihayo Msikela amesema baada ya agizo la IGP Sirro mafanikio hayo yamepatikana.
"Kati ya watuhumiwa hao 40, watuhumiwa 27 wameachiwa huru, lakini 13 tunaendelea kuwashikilia na miongoni mwao wapo walioshiriki mauaji moja kwa moja, wamo waliotoa usafiri na kuitisha vikao," amesema Mihayo.
Aidha mkuu huyo alitoa rai kwa wananchi wote nchi nzima kusalimisha silaha wanazomiliki kihali na kuzitumia katika uhalifu na zile ambazo wanamiliki isivyo halali, vinginevyo baada ya siku saba hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.