Ajali ya treni yaua wanne na kujeruhi 132 Tabora

Muktasari:

  • Watu wanne wamefariki na wengine 132 kujeruhiwa katika ajali ya treni iliyotokea leo Jumatano Juni 22, 2022 katika eneo la Malolo, mkoani Tabora.



Dar es Salaam. Watu wanne wamefariki na wengine 132 kujeruhiwa katika ajali ya treni iliyotokea leo Jumatano Juni 22, 2022 katika eneo la Malolo, mkoani Tabora.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mkuu wa Kitengo cha Habari na Uhusiano wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Jamila Mbarouk imeeleza kuwa treni hiyo iliyokuwa ikisafiriki kutoka Kigoma kuelekea Dar es Salaam imepata ajali hiyo saa 5:00 asubuhi.

Taarifa hiyo imetaja waliofariki ni mtoto wa kike (5), wakiume (miezi minne), mwanaume mmoja na mwanamke mmoja ambao umri wao haujawekwa wazi.

“Treni hiyo ilikuwa na behewa nane zilizobeba abiria 930, majeruhi 132 tayari wamepelekwa katika Hospitali ya Mkoa, Kitete- Tabora na wanaendelea vizuri.

“Ilipofika eneo la Malolo, behewa tano za abiria daraja la tatu, moja la vifurushi, moja la huduma ya chakula na vinywaji zilianguka na kusababisha ajali,” imeeleza taarifa hiyo.