Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Aliyeponzwa na lifti, akatupwa jela miaka 20 aachiwa huru

Dar es Salaam. Mfanyabiashara wa jijini Dar es Salaam, Haika Mgao, ambaye mwaka 2019 alihukumiwa kifungo cha miaka 20 jela kwa kukutwa na vipande vinne vya meno ya tembo na meno mawili ya kiboko, ameachiwa huru baada ya kushinda rufaa.

Ushindi wake umekuja, huku Maria Ngoda, mkazi wa Isakalilo wilaya ya Iringa aliyefungwa miaka 22 jela kwa kupatikana na vipande 12 vya nyama ya swala akiwa katika mchakato wa kukata rufaa kupinga hukumu hiyo.

Muda wote wa kesi, Haika alikiri kuwepo kwenye gari lililokuwa likiendeshwa na Anthony Chibarangu na kwamba, alipewa tu lifti kutoka Kimara kwenda Manzese alikokuwa anaenda kumsalimia rafiki yake wa kiume.

Novemba 19, 2019 wakiwa Kimara jijini Dar es Salaam, gari alilodai kupewa lifti lilikamatwa na polisi na katika upekuzi lilikutwa na vipande vitatu vya meno ya tembo vyenye thamani ya Sh66.2 milioni na meno ya kiboko yenye thamani ya Sh3.3 milioni.

Hata hivyo, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Godfrey Isaya hakuamini hadithi yake na kumtia hatiani na kumhukumu kifungo cha miaka 20 jela kwa kila kosa kwa makosa matatu, lakini aliamuru atumikie vifungo hivyo kwa pamoja.

Januari 4, 2024, jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, Dk Gerald Ndika, Ignas Kitusi na Lilian Mashaka katika hukumu yao lilibatilisha adhabu hiyo na kuamuru aachiwe mara moja kutoka gerezani anakoshikiliwa.
 

Ushahidi ulivyokuwa

Ushahidi wa upande wa Jamhuri ulieleza maofisa wanyamapori walikuwa wana taarifa fiche kutoka kwa msiri wao, ambao nao waliwajulisha polisi kwamba kuna watu huko Kimara walikuwa na nyara za Serikali, hivyo msaada wa polisi ulihitajika ili kuwakamata.

Shahidi wa kwanza, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Salum Malugugile aliweka mtego ambao aliendesha gari la kiraia akiwa na Koplo John na Konstebo Ayubu ambao waliongozana na ofisa wanyamapori Abel Joel, aliyekuwa amewapa taarifa.

Kulingana na ushahidi huo, Abel alikuwa na namba za washukiwa ambao aliwapigia simu na kuwajulisha kuwa amefika, akijifanya ni mnunuzi wa meno ya tembo.

Watu watatu walijitokeza na baada ya kukubaliana, walienda kuleta meno hayo.

Hata hivyo, kulingana na ushahidi huo, ni watu wawili waliorejea ambao ni mwanamke na mwanamume wakiwa wamebeba begi na wakatakiwa kulifungua ili ‘wanunuzi’ hao wajiridhishe.

Inspekta Malugulile alikuwa tayari amewatonya wenzake, hivyo timu ya maofisa wenzake ilimkamata Anthony Philemon na Haika.

Kwa upande wake, shahidi wa pili, Said Ng’anzo ambaye ni ofisa wanyamapori alitambua nyara hizo, kuzipima na kutoa thamani yake. Shahidi wa tatu, alitajwa kwa jina la Josephine aliyeandika maelezo ya onyo ya Haika.


Jinsi alivyojitetea kortini

Katika utetezi mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Haika alikiri kuwa katika gari lililokuwa likiendeshwa na Anthony Chibarangu na kwamba alipewa tu lifti kutoka Kimara anakoishi kwenda Manzese kumtembelea rafiki yake wa kiume.

Njiani gari hilo lilisimamishwa na maofisa wa Jeshi la Polisi ambao waliwaweka chini ya ulinzi. Alikana kusaini hati ya kukamata mali eneo la tukio bali alitakiwa kuisaini Mikocheni katika ofisi za kikosi kazi cha kupambana na ujangili.

Pia alikanusha kutoa maelezo ya onyo ya kukiri kosa mbele ya shahidi wa tatu wa upande wa mashitaka na kwamba, hakuwahi kuulizwa swali lolote linalohusu kutenda kosa linalomkabili na maelezo yaliandikwa nje ya muda.

Mahakama iliridhika kuwa ingawa shahidi pekee ambaye ni wa kwanza wa upande wa mashitaka ndiye aliyetoa ushahidi kwamba alikutwa na meno hayo, iliona ushahidi wake ni bora kuliko hata kuwa na mashahidi wengi, hivyo kuamua kumtia hatiani.

Hakimu alimhukumu kifungo cha miaka 20 kwa kila kosa na kwa makosa matatu, alihukumiwa kwenda jela miaka 20 kwa kuwa vifungo vyote vingetumikiwa kwa pamoja.
Alikata rufaa Mahakama Kuu lakini ikatupwa.
 

Majaji walivyochambua

Katika kesi ya rufaa iliyowasilishwa Mahakama ya Rufaa, majaji watatu walisema maelezo ya onyo ya mshitakiwa yaliwahi kutolewa katika kesi ya uhujumu uchumi namba 36 ya 2015 dhidi ya Haika, lakini Mahakama iliyakataa.

“Tunavyoona jaji hakuifanyia kazi vizuri hoja ya maelezo hayo, bali alirahisisha mambo. Kama hakimu mkazi mmoja katika mahakama hiyohiyo alisema hayastahili kupokewa kama kielelezo alitakiwa naye alione hilo ilipoletwa mara ya pili,” inaeleza sehemu ya hukumu.

“Tunaona kuwa uamuzi wa mahakama hizo mbili (Mahakama Kuu na Mahakama ya Hakimu Mkazi) kuhusu kupokea maelezo hayo kama kielelezo haikuwa sahihi, kwa hiyo tunaifuta kwenye mwenendo wa kesi hii,” inaeleza hukumu.

Kuhusu ushahidi wa shahidi wa kwanza ambao mahakama za chini ziliona unaaminika na ndio ambao ulimtia hatiani pia, jopo la majaji walijiuliza ilikuwaje hadithi ya shahidi huyo pekee iliaminika lakini ya mrufani (Haika) haikuaminika.

“Swali la pili ni kwa nini Abel Joram, ofisa wanyamapori aliyeshiriki sana hadi kuandaa mtego siku ya tukio hakutoa ushahidi kwenye kesi. Swali lingine ni kwa nini Anthony Philemon ambaye ni mtuhumiwa wa pili hakushitakiwa pamoja na Haika,” walihoji majaji katika hukumu hiyo.

“Kwa maoni yetu, Mahakama Kuu ilifanya kosa kwa kutofanyia upya uchambuzi wa ushahidi kwa sababu ni wajibu wa mahakama kama chombo cha kwanza cha rufaa kufanya hivyo. Hii inatufanya tuvae viatu vyao na kuona hoja tatu za rufaa zina mashiko,” nasema hukumu hiyo.

“Tunatilia shaka uaminifu wa ushahidi wa shahidi wa kwanza kwa sababu hakueleza kwa vipi Anthony Philemon anayeonekana hadi kwenye cheti cha ukamataji mali alipotelea hewani. Kuacha kumshitaki mshirika wake kunaleta shaka,” inaeleza hukumu.

Majaji katika hukumu wanaeleza, “Kama shahidi huyo wa kwanza angekuwa mwaminifu angeiambia mahakama nini kilitokea kwa Anthony Philemon (ambaye walikamatwa pamoja na Haika) ambacho kiliwazuia polisi au chombo kingine cha dola kumshitaki.”

Majaji walisema kwa kuwa maelezo ya kukiri kosa yameshaondolewa kwenye mwenendo wa shauri hilo, uaminifu wa ushahidi wa shahidi huyo wa kwanza unapoteza nguvu, hasa kwa kuwa upande wa mashitaka uliacha kuita mashahidi wengine muhimu.