Chande: Si busara kushusha bei ya umeme

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akimsikiliza, Waziri wa Nishati, January Makamba pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Maharage Chande kuhusiana na kituo cha kusafirishia umeme (Switchyard) katika Mradi wa Bwawa la kuzalisha umeme (Megawati 2,115) la Julius Nyerere (JNHPP) katika Mto Rufiji Mkoa wa Pwani. 

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Maharage Chande amesema hadhani kama ni busara kushusha bei ya umeme baada ya mradi wa kuzalisha umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) kuanza uzalishaji.

Chande amebainisha hayo leo Mei 26, 2023 wakati akijibu swali na Mhariri Mtendaji wa gazeti la Nipashe, Beatrice Bandawe aliyetaka kujua kama bei ya umeme itashuka baada ya mradi huo kuanza uzalishaji.

Amesema huwezi kushusha bei ya umeme baada ya kuanza kuzalisha JNHPP wakati hata miundombinu inayojengwa kwa kutumia mapato yanayotokana na uuzwaji wa umeme haijakamilika.

"Mimi sidhani kama ni busara kushusha bei ya umeme ili fedha tutakayobaki nayo ibaki kuhudumia umeme. Hapa ni vizuri kutofautisha bei na gharama, ni vitu viwili tofauti," amesema Chande.

Mkurugenzi huyo ameongeza kwamba ukitaka kukua, usishushe bei ya umeme, bali ubaki vile vile ili yale mapato yatumike kujenga miundombinu na kuendelea kuzalisha umeme.