CRDB yashinda tuzo ya Benki Bora Tanzania
Muktasari:
Benki ya CRDB inajivunia kutunukiwa tuzo ya Benki Bora nchini kwa mwaka 2022 na Jarida la Euromoney.
Benki ya CRDB inajivunia kutunukiwa tuzo ya Benki Bora nchini kwa mwaka 2022 na Jarida la Euromoney.
Ikiwa ni tuzo yake ya pili kuinyakua, baada ya kushinda tuzo kama hiyo kwa mara ya kwanza mwaka 2004, ushindi huo haukuwa wa kubahatisha bali jitihada na mikakati ya benki hiyo.
Furaha isiyo kifani imemsogeza karibu Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela ambaye anakiri kuwa, “Tuzo ya Euromoney inathibitisha nafasi ya CRDB kama benki inayoongoza nchini.
Pia inatambua mafanikio ya mageuzi ambayo yamesababisha ukuaji endelevu wa benki yetu na kunufaisha wateja wetu, wawekezaji na uchumi wa nchi kwa ujumla,” Nsekela aliongeza.
Anasema kuwa mafanikio hayo ya katikati ya mwaka yanaakisi mwenendo mzuri wa benki uliowezesha ukuaji endelevu wa tarakimu mbili katika kipindi cha miaka minne iliyopita ikichagizwa na mageuzi ya kimkakati na uvumbuzi.
Pia anaelezea kuongezeka kwa kiwango cha faida cha benki hiyo kwa miaka miwili iliyopita ambapo faida baada ya kodi iliongezeka kutoka Sh165.2 bilioni mwaka 2020 hadi kufikia Sh268.2 bilioni mwaka 2021.
Hii ndiyo faida kubwa zaidi katika historia ya benki na hiyo inadhihirisha thamani ya mageuzi endelevu ambayo benki imeyafanya katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Kulingana na Nsekela, vipimo vingine muhimu vilivyoupa ushindi benki hiyo ni uendelevu wa uzalishaji wa thamani kwa wanahisa wake (na washikadau wengine) kupitia mapato endelevu.
Pia imekuwa taasisi inayoongoza kibiashara kusaidia minyororo ya thamani ya kiuchumi inayoendelea kuboresha maisha ya Mtanzania mmoja mmoja na uchumi.
“Katika eneo la ubunifu, benki inaendelea kushika usukani wa soko la Tanzania, ubunifu katika kubadilisha maisha katika sekta ya huduma za fedha katika nyanja ya malipo na bidhaa zilizoboreshwa.
Benki pia inajivunia kuwa kinara katika kutengeneza masuluhisho ya fedha kwa minyororo maalum ya thamani kulingana na mpango wa uchumi wa nchi,” anaarifu.
Benki hiyo inaonyesha ukubwa wake wa mizania ya Sh 9.4 trilioni kama kichocheo chake cha kiuchumi mbali na kuwezesha sekta muhimu za uchumi kama vile; kilimo, miundombinu, viwanda na utalii, miongoni mwa mambo mengine.
Mafanikio ya Benki ya CRDB vilevile yanachagizwa na kampuni yake tanzu ya CRDB Burundi ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika biashara yake katika kipindi cha miaka 10 toka kuanzishwa kwake.
“Benki itaendelea kutanua wigo wake na hivi karibuni inatarajia kuingia katika soko la Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC) kurahisisha ufanyikaji wa biashara baina ya Tanzania na DRC ukizingatia nchi hiyo inategemea bandari ya Dar es Salaam kwa uuzaji na ununuaji wa bidhaa,” anafafanua zaidi.
Kwa upande mwingine, Nsekela anaeleza kuwa Benki ya CRDB ni benki ya kwanza ya biashara Afrika Mashariki iliyoidhinishwa na Mfuko wa Hali ya Hewa ya Kijani (GCF) kama taasisi mwezeshaji wa uboreshaji wa mazingira nchini.
Akielezea zaidi kauli hiyo hapo juu, anasema kuwa pia ni Taasisi ya kwanza miongoni mwa zile zilizochaguliwa na Mfuko wa GCF kupata kibali cha ufadhili wa mradi wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi na teknolojia ya kilimo unaolenga kuboresha kaya zaidi ya milioni sita Tanzania.
Pia, Benki ya CRDB ni balozi wa masuala ya mazingira nchini kupitia Mradi wa ‘Pendezesha Tanzania’ ambao unalenga kutunza mazingira kupitia upandaji miti, usafi wa miji na nishati endelevu.
Nini maana ya Euromoney?
Euromoney ni jarida la kimataifa linalochanganua data kutoka kwa kampuni zote duniani na kutambua biashara zinazofanya vizuri zaidi ikiwemo benki za biashara.
Euromoney imekuwa ikifanyia tathmini taasisi za fedha zinazoongoza ulimwenguni kupitia takwimu za kiutendaji, tafiti na tuzo ilizowahi kushinda kwa zaidi ya miaka 25 katika eneo la huduma za kibenki.
Tuzo za kila Mwaka za Ubora (AAEP), zilianzishwa mwaka 1992 na kuvutia ushiriki wa zaidi ya benki 1,200 viongozi duniani kote. Tuzo hizo zinatambua ubora katika vipengele vya kimataifa, kikanda na nchi binafsi.
Euromoney ipo katika zaidi ya nchi 160 na zaidi ya wafanyakazi 2,500 walio Amerika Kaskazini, Amerika Kusini, Ulaya na Asia.
Namna utaratibu ulivyokuwa?
Pamoja na jukumu lake la kupima na kutunuku tuzo za ubora wa benki, kamati ya Tuzo hizo za AAEP ilifanya mapitio ya utendaji wa benki hiyo, dhidi ya mkakati wake na eneo ambalo benki hiyo inaendesha shughuli zake ndani ya Tanzania na Afrika Mashariki.
Utengenezaji wa thamani wa benki na mchango wake katika maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania na Burundi pia uliiongezea alama benki hiyo katika kinyang’anyiro hiko.
Ushindi huu una maana gani kwa Benki ya CRDB?
Hatua iliyofikiwa inamaanisha uwepo wa ari ya hali ya juu ya benki katika kuchochea ukuaji zaidi unaosimamiwa na mikakati thabiti na ya kimaendeleo iliyopangwa na benki.
Ni fursa ya benki kujiweka karibu zaidi na dunia, kutanua wigo wa bidhaa, ushiriki wa jamii na uvumbuzi wa hali ya juu.
Benki ya CRDB inajivunia mafanikio hayo lakini haiwezi kubweteka kwa hatua na badala yake ni mwanzo wa safari nyingine ya mafanikio zaidi.