Hiace yapinduka, yaua nane Bukoba

Hiace yapinduka, yaua nane Bukoba

Muktasari:

Chanzo cha ajali hiyo ni  mwendo kasi na kwamba baada ya dereva   kuona gari lina hitilafu na kushindwa kulimudu, alilishusha chini kwenye mteremko mkali ng'ambo ya barabara ambako kuna shimo la maporomoko ya maji.

Bukoba. Watu wapatao nane wamepoteza maisha na wengine sita kujeruhiwa katika ajali ya gari la abiria lenye namba za usajili T.471 DCG linalofanya safari za kubeba abiria kutoka Kemondo  kwenda  Bukoba Mjini,  baada ya gari hilo kufeli breki na kupinduka.

Ajali hiyo ilitokea Novemba 22 saa 1:45 usiku na  gari hilo aina ya  Toyota Hiace yenye namba za usajili T. DCG lilikuwa likiendeshwa na Ismail Rashid (37) mkazi wa Kemondo.

Mmoja wa majeruhi  wa ajali hiyo Johanes Gilbert, amesema akiwa barabarani kutokea fukwe za Ziwa Victoria kabla ya kupata ajali aliona gari ikitokea upande wa juu kushuka chini aliendelea kutembea usawa wa gari hilo ambapo baadaye alijikuta hospitali bila kujua amefikaje akiwa ameumia jicho na kidevu.

Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya rufaa Bukoba, Charles Kahigi  alisema Novemba 22 usiku walipokea miili sita ya marehemu  na baadaye  kuongezeka wawili na majeruhi sita.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kagera, Revocatus Malimi alisema kuwa baada ya ajali hiyo watu watano walikufa papo hapo ambapo wawili walikuwa ni watembea kwa miguu na watatu walikuwa abiria na majeruhi walipelekwa hospitalini ambapo wakati majeruhi wakiwa mapokezi mmoja alipoteza maisha.

Alisema chanzo cha ajali hiyo ni  mwendo kasi na kwamba baada ya dereva   kuona gari lina hitilafu na kushindwa kulimudu, alilishusha chini kwenye mteremko mkali ng'ambo ya barabara ambako kuna shimo la maporomoko ya maji.