Jela maisha kwa kumbaka mtoto wa miaka saba Nkasi

Muktasari:

  • Mkazi wa Namanyere, Wilaya Nkasi mkoani Rukwa, Athanas Exavery (32) amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mtoto wa kike mwenye miaka saba.

Nkasi. Mahakama ya wilaya Nkasi mkoani Rukwa imemhukumu kifungo cha maisha jela mfanyabiashara wa mjini Namanyere, Athanas Exavery (32) baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kumbaka mtoto wa kike wa miaka saba.

 Akitoa hukumu hiyo leo Alhamisi Oktoba 20, 2022 Hakimu Mkazi Mwandamizi Mfawidhi wa mahakama Hhiyo, Denis Luwungo amesema kuwa mahakama imemkuta na hatia mtuhumiwa chini ya kifungu cha 130 (1) cha 2 (e) na kifungu cha 131 (3) cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16.

Amesema kuwa mahakama imejiridhisha pasipo shaka kwamba baada ya upande wa mashitaka kuleta ushahidi wa mashahidi sita na vielelezo sita na kumkuta na hatia hivyo imemhukumu kifungo cha maisha jela.

Awali, upande wa mashtaka ukiongozwa na mwendesha mashtaka wa Jeshi la Polisi, mkaguzi msaidizi Denis Chagike uliieleza mahakama kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo Septemba 11 na 12 katika soko la Majengo mjini Namanyere.

Mwendesha mashtaka huyo aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mtuhumiwa huyo mwenye kesi namba 118 ya mwaka 2021 ili iwe fundisho kwa wengine licha ya kuwa mtuhumiwa huyo ni kosa lake la kwanza.

Akiongozwa na Wakili Peter Kamyalile katika utetezi wake aliiomba mahakama impunguzie adhabu kwa sababu mtuhumiwa bado ni kijana na taifa linamhitaji ikiwa ni pamoja na kwamba anategemewa na familia yake lakini kwa kuzingatia ukubwa wa kosa, mahakama imetoa hukumu hiyo.