Kati ya wasanii hawa mmoja atajiunga WCB

Muktasari:

Hadi sasa WCB imetambulisha wasanii wakubwa watano, lakini inaonekana bado wana kiu ya kupata msanii mwingine

Dar es Salaam. Hadi sasa WCB imetambulisha wasanii wakubwa watano, lakini inaonekana bado wana kiu ya kupata msanii.

Mkurugenzi wa WCB, Diamond Platnumz ameshaweka wazi mpango wake wa kumtambulisha msanii mpya wa kike mwaka 2019.

Wapo wasanii wengi wa kike wanaotarajiwa kujiunga na lebo hiyo miongoni mwao ni Zuchu.

Msanii huyo anatajwa kwa sababu mameneja wa  Diamond akiwamo Hamis Tale maarufu Babu Tale aliwahi kunukuliwa akisema watapenda kuwa na msanii mwenye uwezo mkubwa wa kuimba kama msanii Ruby.

Mwimbaji huyo ana uwezo kutokana na kufanya jingo nyingi za Wasafi Tv na redio kwa ustadi mkubwa, pia alipofanya kava ya nyimbo  za Mbosso ‘Nadekezwa’ na ‘Maajabu’.

Pia amekuwa karibu na familia ya WCB, huku mkurugenzi wa WCB akiwa na ukaribu na mama yake Zuchu  ambaye ni mwibaji taarabu wa malkia wa muziki huo nchini Tanzania, Khadija Kopa.

Mwingine anayekisiwa kusainishwa mkataba ni Tanasha Dona mpenzi wa Diamond.

Licha ya uhusiano walionao, Donna ni mwimbaji mzuri na nyimbo zake zinafanya vizuri kwenye vituo vikubwa vya runinga.

Dona ana nyimbo kali ikiwamo Radio aliomshirikisha  Barak Jacuzzi aliyoitoa Aprili, 2019.

Msanii mwingine anaweza kuwa Precious Marry aliyewahi kutamba katika wimbo wa Dogo Janja wa Wayu Wayu

Huenda pia akawa Gigy Money licha ya mwenyewe mara kadha akusikika akisema hataki kufanya kazi chini ya lebo yoyote.

Nandy naye anaweza kuwa miongoni mwa msanii atakayesainiwa WCB kutokana na kuwa karibu na Diamond.

Nandy ana uwezo wa kuimba lakini ana wafuasi wengi na kwa sifa wanazozitaja WCB  ikiwamo uwezo, anafiti kila idara.

Mbali ya wasanii wa kike pia anatajwa msanii Hans Stone ambaye ni mjukuu wa Khadija Kopa. Msanii huyo aliwahi kusema anavutiwa na Diamond.