Maambukizi Ebola yaongezeka Uganda

Muktasari:

  • Maambukizi na vifo vitokanavyo na ugonjwa wa Ebola vimeanza kuongezeka nchini Uganda ambapo saa 24 tangu kutangazwa kwa mlipuko wa ugonjwa huo imeripoti vifo viwili.



Dar es Salaam. Maambukizi na vifo vitokanavyo na ugonjwa wa Ebola vimeanza kuongezeka nchini Uganda ambapo saa 24 tangu kutangazwa kwa mlipuko wa ugonjwa huo imeripoti vifo viwili.

Licha ya watu sita ambao walifariki wakihisiwa kuugua ugonjwa huo, mpaka sasa Uganda imetaja wagonjwa wapya 11 wa Ebola ambao wamegundulika saa 24 zilizopita huku wengine 10 wakihisiwa ambapo sampuli zimepelekwa maabara.

Ripoti iliyotolewa leo Alhamisi, Septemba 22, 2022 na Wizara ya Afya nchini Uganda imeonyesha mwenendo wa ugonjwa huo ambao hata hivyo mpaka mtu aanze kuonyesha dalili huchukua mpaka siku 21 tangu kupata maambukizi.

“Kwa saa 24 zilizopita, kuna kifo kimoja kutoka wilaya ya Kyegegwa mgonjwa ambaye alikuwa ametengwa katika hospitali ya Rufaa Mubende. Mpaka sasa kuna vifo viwili ambavyo tumethibitisha vimetokana na Ebola na sita vinahisiwa kuwa vilitokana na Ebola kwakuwa watu hawa walifariki wakiwa nyumbani,” imeeleza taarifa hiyo.

Mlipuko wa ugonjwa Ebola mara ya mwisho ulitokea Mashariki mwa Congo ambapo ulianza Agosti 2018 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 1,800 na kuathiri watu 28,616 katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone ukiwa ni mlipuko wa nane kutoka mlipuko wa kwanza mwaka 1976.

Kumekuweko kwa milipuko minne nchini Uganda na mara ya mwisho Uganda iliripoti mlipuko mwaka 2021.

Ebola ni nini

Ebola ni ugonjwa hatari unaosababishwa na kirusi kiitwacho ebola. Kirusi hicho ni moja kati ya familia ya virusi watatu toka katika familia ya filoviridiae.

Zipo aina tano za kirusi cha ebola ambao nao ni bundibugyo ebolavirus (BDBV), zaire ebolavirus (EBOV), reston ebolavirus (RESTV), sudan ebolavirus (SUDV) na tai forest ebolavirus (TAFV).

Aina hizo tatu za virusi, yaani BDBV, EBOV na RESTV, ndiyo inayongoza kwa kusababisha mlipuko wa ugonjwa huo barani Afrika. Hatari ya mgojwa kupoteza maisha ni asilimia 90.